CUF yatoa msimamo, kuhusu wabunge wanaomuunga mkono Maalim Seif

Katibu Mkuu mpya wa Chama Cha Wananchi CUF, Khalifa Suleiman Khalifa amesema chama chao hakina haja ya kuungwa mkono na wabunge wake ambao walikuwa upande wa Maalim Seif kwa kile alichokidai hata wakati wa mgogoro huo walikuwa hawaungwi mkono.

Khalifa Suleyman ametoa kauli hiyo wakati akizungumza kwenye kipindi cha East Africa Breaks cha East Africa Radio ambapo amesema kwa sasa wapo kwenye ujenzi wa chama chao hivyo hawahitaji tena migogoro na wako tayari kufanya kazi na Mbunge yeyote akiomba msamaha.

"Sisi hatuwahitaji wabunge kiasi hicho, kwa sababu tulienda kipindi cha mgogoro hawajatusaidia chochote walitutukana na walitudhalilisha ila sisi tunasema yameshaisha, tujenge chama.

"Watu wenye mtihani mkubwa kwa sasa ni wabunge wa CUF, mimi nafikiri wanapaswa kuwa na busara sana, kwa upande wetu wabunge wametuumiza sana, wabunge wametumia pesa zao kutuumiza sana sisi tunaomuunga mkono Lipumba." amesema Khalifa

Mgogoro wa Chama Cha Wananchi (CUF) umedumu kwa zaidi ya miaka 3, mpaka pale Mahakama ilipotoa uamuzi kuwa Profesa Ibrahim Lipumba ndiye Mwenyekiti halali wa chama hicho na kupelekea aliyekuwa Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif kuhamia ACT - Wazalendo.


from MPEKUZI

Comments