Waziri Mkuu Awataka Vijana Waanzishe Mashamba ya Michikichi

WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amewataka vijana mkoani Kigoma waanzishe mashamba ya michikichi kwa kuwa zao hilo litawapatia kipato cha uhakika.

Amesema Serikari imedhamiria kufufua zao la michikichi ili kuliwezesha Taifa kujitosheleza kwenye mafuta ya kula na kuokoa fedha za kigeni.

Ameyasema hayo leo (Jumatatu, Februari 18, 2019) alipowasalimia wananchi wa kijiji cha Nyakitondo wilayani Kasulu akiwa njiani kwenda Kibondo.

Waziri Mkuu ambaye yupo mkoani Kigoma kwa ziara ya kikazi yenye lengo la kufufua kilimo cha michikichi amesema ni vema wananchi wakachangamkia fursa hiyo.

“Vijana limeni michikichi kwani ukipanda ukiwa darasa la tano baada ya miaka mitatu utaanza kuvuna na kujipatia kipato ambacho kitakuwezesha kujikimu.”

Amesema kilimo cha zao la michikichi kitawawezesha wananchi hususani vijana kupata mitaji ya uhakika kwa ajili ya shughuli zingine za kiuchumi

Hata hivyo, Waziri Mkuu amesema Serikali imejipanga kuhakikisha Tanzania inaongoza kwa kilimo cha zao la michikichi katika nchi za Afrika Mashariki.

Kadhalika, Waziri Mkuu amewahamasisha wananchi hao wajiunge na Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) ili wawe na uhakika wa matibabu kwa yao na familia zao.

Wakati huohuo Waziri Mkuu ametembelea kambi ya Wakimbizi ya Nduta wilayani Kibondo na kukagua shule ya msingi Kassim Majaliwa na baadae wodi ya wazazi katika Hospitali Nduta.

 (mwisho)
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU


from MPEKUZI

Comments