Watu Wawili Wapandishwa Kizimbani Kwa Kukutwa na Kilo 14 za Bangi

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kinondoni, Dar es Salaam imewapandisha kizimbani watu wawili kwa shtaka la kukutwa
na dawa za kulevya aina ya bangi zenye uzito wa kilo 14.07.
 
Waliopandisha kizimbani ni Musa Amos (19) mkazi wa Tandale Sokoni na Anas Swalehe (18) mkazi wa Magomeni Kagera.
 
Wakisomewa shtaka hilo mbele ya Hakimu Karoline Kiliwa, Mwendesha mashtaka wa Jamhuri, Grace Lwila, alidai Novemba 26 mwaka jana, eneo la Tandale kwa Mtogole, Wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam, washtakiwa walikutwa na dawa hizo huku wakijua ni kinyume cha sheria.
 
Washtakiwa walikana kutenda kosa hilo na Hakimu Kiliwa alisema dhamana iko wazi kwa wadhamini kutoa bondi ya Sh 100,000 kwa kila mmoja.
 
Hata hivyo walishindwa kukidhi masharti ya dhamana na kurudishwa rumande hadi kesi yao itakaposomwa tena Januari 30.


from MPEKUZI

Comments