Watalii 61 Wawasili Nchini Kwa Treni

Na Paschal Dotto-MAELEZO.
Watilii 61 kutoka nchi mbalimbali wamewasili Jijini Dar es Salaam leo kutoka Afrika ya kusini kwa kutumia treni ya kifahari ya Rovos,kwa nia ya kuja kuangalia vivutio vya kitalii vinavyopatikana hapa nchini.

Akizungumza katika mapokezi hayo Meneja Uhusiano wa Bodi ya Utalii nchini Geofrey Tengeneza amesema kuwa kupokelewa kwa wageni hao ni fahari kwa Bodi ya Utalii  kwani ni mwanzo mzuri wa kupata mabalozi wa kuitangaza Tanzania katika sekta ya utalii duniani.

“Tupo hapa kuwapokea watalii hawa 61 kutoka nchi mbalimbali duniani wakitokea Afrika ya Kusini wakitumia Treni hii ya kifahari (ROVOS) Pride of Afrika iliyosafiri kwa siku 15 ikitokea Cape Town mpaka Dar es Salaam ikiwa ni mara ya kwanza kuwasili nchini  kwa mwaka huu wa 2019.”, Alisema Bw.Tengeneza.

Alisema kuwa katika kundi hilo la watalii wapo Waingereza, Wajerumani, Waholanzi, Wasweden, Waitaliano pamoja na watalii kutoka Afrika ya Kusini, treni hiyo imekua ikija nchini mara tano kwa mwaka.

“Nifahari kwa Bodi ya Utalii na Sekta ya Utalii kwa ujumla nchini kwani itaongeza idadi ya watalii wanaowasili nchini kwakutumia hawa 61 kusambaza mema na vivutio vilivyoko Tanzania, lakini pia imeweka uhusino mzuri na watu wa ROVOS kufanya safari zao Dar es Salaam Tanzania mpaka Cape Town Afrika ya Kusini”, alisema.

Tengeneza alisema kuwa katika kundi la watalii hao 61 watagawanyika na kwenda sehemu mbalimbali za kitalii zikiwemo Zanzibar, Serengeti, Ngorongoro pamoja na sehemu nyingine za utalii hasa zinazopatikana Dar es Salaam na Maeneo ya Jirani kama vile Bagamoyo na Saadani.

Treni hii ambayo imekuwa na utamaduni wa kuwasili nchini kupitia reli ya TAZARA imekuwa na ratiba ya kuja nchini mara 5 kwa mwaka huku ikipita katika nchi mbalimbali kama vile  Zimbabwe, Botswana na Zambia na kuingia Tanzania kupitia mpaka wa Tunduma na kupita maeneo mbalimbali ya kitalii ikiwemo Selous.

Watalii hawa watakaa nchini kwa siku 7 huku Treni ikitarajia kuondoka tarehe 24 Januari 2019 ikiwa na watalii wengine ambao walikuja mapema kwa kutumia usafiri wa ndege.


from MPEKUZI

Comments