Wadau waeleza madini yanavyotoroshwa kwenye matikiti maji

Wadau wa madini wameeeleza jinsi madini nchini yanavyotoroshwa kwenda nje ya nchi kupitia mipakani.

Wadau hao wameeleza hayo leo Jumanne Januari 22, kwenye Mkutano wa Kisekta wa Wizara ya Madini ulioshirikisha wadau mbalimbali wa madini, baada ya Rais John Magufuli kutoa nafasi kwa wadau hao kuelezea changamoto zinazowakabili.

Mmoja wa wadau wa madini kutoka mkoani Geita, amesema madini hayo hutoroshwa na watu kutoka nje ya nchi kwa kutumia mbinu mbalimbali ikiwamo kuficha kwenye matikiti maji.

“Mtu anaweza akaiba dhahabu na kuweka hata kwenye ‘side mirror’, tikiti maji, kabichi, au tairi la spea, kwenye tikiti maji na kabichi anakata anaingiza kilo nyingi tu za dhahabu.

“Tukipata nafasi ya kuzungumza kwa utaratibu tutayasema haya yote, serikali inatoa taarifa ambazo sio sahihi ndiyo maana uliposema tujadili watu walipiga makofi.

“Pale Uwanja wa Ndege wa Mwanza, zile mashine ukienda na karatasi za namna fulani ukafunga madini unapita bila usumbufu wowote, nilienda kwenye kamati na tukakubaliana kwenda kuhakikisha na tulipofika ni sehemu moja tu ilionyesha kuna madini lakini sehemu nyingine hazikuonyesha,” amesema.

Mchimbaji huyo mdogo wa almasi, amesema utoroshwaji  madini unachangiwa kwa kiasi kikubwa na wanunuzi wa ndani kunashindwa kumudu ukubwa wa ada za leseni ambazo huhitaji zaidi ya Sh5 milioni.

“Tulikuwa tunaomba kwa sisi kama wazawa angalau iwe Sh2 milioni, kwa wageni hata ikiwekwa Dola 5,000 za Marekani haina shida,” amesema.

Mjumbe wa Melema tawi la Mirerani, Fatuma Kikuyu amesema vijana walio nje ya ukuta ni wengi kuliko waliopo ndani  kutokana na kukosa mikataba na kulipa mishahara.

“Ungetuachia lile geti la Magufuli wazi ili vijana waingie kwenda kufanya kazi ili kuopngeza pato la taifa, jambo ambalo linawasababisha kuruka ukuta hivyo tunaomba tufanye kazi kama zamani,” amesema Fatuma.


from MPEKUZI

Comments