DRC: Polisi yamzuia Fayulu kuhutubia wafuasi wake....Bado Anasisitiza Yeye Ndo Mshindi Halali wa Urais

Polisi wamezuia wafuasi wa Martin Fayulu kukusanyika kwenye makao makuu ya chama chake alitakorajiwa kuwahutubia. Ingawa Korti ya Katiba imethibitisha ushindi wa Felix Tshisekedi, Fayulu anadai ameibiwa ushindi wake.

Msemaji wa Martin Fayulu Eve Bazaiba amesema polisi walivamia mahali ambako Fayulu alikusudia kuwahutubia wafuasi wake, na kulibeba jukwaa na vipazasauti vilivyokuwa vimeandaliwa.

''Wamevikamata vyombo vyote na kuwakamata pia watu, na sijui wamewapeleka wapi.'' amelalamika Bazaiba na kuongeza, ''nilipouliza kinachoendelea, nimeambiwa polisi wanacho kibali cha kuwazuia watu kuingia na kutoka.''

Licha ya kutawanywa na polisi baadhi ya wafuasi wa vuguvugu la upinzani la LAMUKA linalomuunga mkono Fayulu waliendelea kusubiri kuwasili kwa kiongozi wao kwenye makao makuu ya chama cha MLC.

Fayulu na wafuasi wake ambao wamepinga matokeo yaliotolewa na tume ya uchaguzi na kujitangaza kuwa mshindi wa uchaguzi huo amesema kwamba ni lazima raia wa kongo wapewe haki zao.

''Tunachotaka ni kupata haki kulingana na matokeo ya uchaguzi, kwa sababu tuna uhakika kwamba tulishinda,'' amesema msemaji wa Fayulu Eve Bazaiba, na alipoulizwa watafanya nini kuhakikisha wanafanikiwa, amesema watazidi kukazana kwa sababu 'sheria iko upande wetu.''

Wakati huohuo, mandalizi kwa ajili ya kuapishwa kwa rais mteule Felix Tshisekedi yanaendelea mjini Kinshasa. Sherehe hiyo iliotarajiwa kufanyika Jumanne imeahirishwa hadi Alhamisi, hiyo ikiwa ni kwa mujibu wa Lambert Mende msemaji wa serikali inayoondoka madarakani.

Mahali patakapofanyika sherehe hiyo bado kufahamika, lakini wafuasi wa chama cha UDPS cha Tshisekedi waliomba kiongozi wao aapishwe kwenye uwanja wa kandanda wa Kinshasa ilikuwaruhusu washiriki pia.

Ni kwa mara a kwanza Kongo itashuhudia kuapishwa kwa rais mpya kufuatia kuchukuwa madaraka kwa njia ya amani kutoka kwa rais mwingine.

Credit:DW


from MPEKUZI

Comments