Lugola Atoa Onyo Kali Kwa Wanaojipenyeza Kupitia Taasisi Za Dini Kuhubiri Siasa, Uchochezi

Na Felix Mwagara, (MOHA), MARA.
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola amesema wapo baadhi ya watu ambao wanajipenyeza kupitia mgongo wa taasisi za dini nchini kujifanya wahubiri kumbe ni wachochezi na wanajiingiza katika masuala ya kisiasa.

Amesema Wizara yake ipo makini katika kusajili Makanisa na Misikiti yote nchini na mpaka sasa wana maombi mengi ambayo yametumwa wakiomba kusajiliwa ambapo baadhi yao bado hayajasajiliwa kwasasababu wanahitaji umakini mkubwa katika kufanya uchunguzi wa kina kabla hawajatoa usajili ikiwa na lengo la kuepusha baadhi ya taasisi za dini zenye mpango mbaya na maendeleo ya  nchi.

Akizungumza na mamia ya wananchi wa Kijiji cha Sunsi, Kata ya Nampindi, Jimbo la Mwibara, Wilaya ya Bunda, Mkoani Mara, jana, Lugola ambaye ni Mbunge wa Jimbo hilo, alisema taasisi za dini zina mchango mkubwa nchini na uwepo wao ni muhimu katika maendeleo ya nchi, na serikali inawathamini mchango wao katika kuimarisha amani na pia kuwaweka watu pamoja lakini kuna baadhi ya dini hizo zinakiuka utaratibu wa usajili na kuvunja sheria za nchi kwa kuacha kuhubiri masuala ya kiroho wanajihusisha na masuala ya kisiasa pamoja na uchochezi.

“Serikali ya Rais Dk. John Magufuli ya Awamu ya Tano haitakua tayari kwa mwananchi yeyote kutumia mwavuli wa dini, au kufanya misikiti na makanisa kuwa kichaka kwa kufanya uchochezi katika nchi hii, kuhatarisha amani ya nchi hii, tupo makini na hatuwezi kuchezewa na mtu yeyote au taasisi yoyote,” alisema Lugola.

Lugola alitumia muda mrefu kutoa ufafanuzi huo baada ya kukaribisha maswali mbalimbali kutoka kwa wakazi wa kijiji hicho katika mkutano huo ili wananchi hao waweze kuuliza ndipo mmoja wao akauliza kuhusu uchelewashaji wa usajili wa kanisa.

“Taasisi hizi za Makanisa na Misikiti wanao mchango mkubwa sana kwa wananchi hususani waumini wao katika kuhubiri amani ya nchi hii, katika kukemea vitendo vya rushwa kwasababu hata katika maandiko rushwa imekemewe, rushwa imeonekana ni hatari katika vitabu vyote vitakatifu vya dini, lakini wapo baadhi ya watu wasiowaaminifu nchini wamejipenyeza na wanaendelea kujipenyeza katika taasisi hizo, na badala ya kuhubiri masuala ya kiroho, wanajihusisha na masuala ya uchochezi na uvunjifu wa amani,” alisema Lugola.

Lugola amesema Serikali haitakubali kuchezewa na kutokana na sababu hizo na nyinginezo Wizara yake inaendelea kuwa makini kuyafanyia kazi maombi ya taasisi hizo kwa kuomba usajili, na aliwataka ambao wametuma maombi yao kwa muda mrefu waendelee kusubiri wakati Serikali ikiendelea kuwa makini kuyafanyia kazi maombi yao.

“Serikali ya Awamu ya Tano haitakua tayari mwananchi yeyote kutumia mwavuli, kufanya misikiti na makanisa kuwa kichaka cha kufanya uchochezi, kuhatarisha amani ya nchi hii, Serikali ya Magufuli  ipo makini sana zaidi mnavyofikiria,” alisema Lugola.

Pia Lugola aliwataka wananchi nchini waendelee kutoa taarifa za uhalifu, taarifa majambazi, vibaka ili Jeshi la Polisi liweze kufanya kazi na waone makali ya Jeshi hilo katika utendaji wa kazi, kwasababu askari waliapa kulinda usalama wa raia na mali zao.

Waziri huyo aliwataka Watanzania waendelee kufanya shughuli zao kwa amani na utulivu kwa kuwa Jeshi lake lipo imara na linafanya kazi usiku na mchana ili kuhakikisha nchi inaendelea kuwa na amani.

Aidha, Waziri Lugola aliwataka wananchi wa jimbo lake waanze maandalizi ya kilimo cha mazao ya chakula na biashara ili kuepuka janga la njaa lisije liwakumba endapo hawata lima.

“Nipo katika ziara hii kwa lengo la kuwahamasisha mwezi huu wa Desemba muanze maandalizi ya kilimo cha mazao ya pamba, mahindi, mpunga, viazi na mengineyo ambapo ndani ya jimbo hili mnayalima,” alisema Lugola.

Lugola ameikamilisha ziara aliyoipanga kwa kutembelea Kata zote za Jimbo hilo kwa kuwapa elimu mbalimbali ya mipango ya miradi ya maendeleo jimboni humo na kuwaahidu kuyafanyia kazi changamoto mbalimbali zinazowakabili.


from MPEKUZI

Comments