Sakata la Korosho: Waziri wa Viwanda Joseph George Kakunda Awatumbua Wakurugenzi wawili

Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, George Kakunda leo Novemba 14 amewavua ukurugenzi wakurugenzi wawili wanaosimamia viwanda na maghala katika wizara hiyo kwa madai ya uzembe uliosababisha kuzorota kwa viwanda vya korosho.

Kakunda aliyeteuliwa hivi karibuni akimrithi, Charles Mwijage amesema baada ya kutembelea viwanda hivyo jana kuanzia mkoani Lindi hadi Mtwara amekuta hali mbaya huku viwanda vingi vikiwa vimegeuzwa kuwa maghala.

"Nimeamua kumpunguzia majukumu ndugu Isaac Legonda, mkurugenzi wa maendeleo ya viwanda, ataripoti kwa Katibu Mkuu atapangiwa kazi nyingine ya uofisa," alisema Waziri Kakunda.

Aliongeza: "Nimemtafuta tangu juzi ili aweze kunipa habari za viwanda hayupo ofisini, Katibu Mkuu hana taarifa za kutosha huyu mtu yuko wapi. Katibu Mkuu atajua mwenyewe hatua zinazotumika katika kanuni za adhabu za utumishi."

Alimtaja pia Augustino Mbulumi ambaye pia ni mkurugenzi wa usimamizi wa maghala na kusema kwamba ametengua uteuzi wake kutokana na utendaji kazi hafifu na uzembe.

"Atateuliwa mkurugenzi mwingine ambaye atakuwa tayari kuwajibika vizuri zaidi. Hatuwezi kuwa na watu ambao hawaendi na kasi ya mheshimiwa Rais," alisema Kakunda.


from MPEKUZI

Comments