Mkongo Wa Taifa Wa Mawasiliano Waongeza Mapato Ya Serikali

Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano umeongeza makusanyo ya mapato ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye maeneo ya mipakani mwa Tanzania na nchi jirani za Rwanda, Uganda, Burundi na DRC Congo

Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye wakati wa ziara yake ya kukagua Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano kwenye kituo cha mpakani cha Mtukula ambacho kinawezesha usafirishaji wa taarifa na data za wateja na bidhaa kutoka Tanzania kwenda nchi jirani ya Uganda.

Nditiye amesema kuwa, “maeneo ya mipakani ndi lango la kuongeza mapato na kukuza uchumi wan chi yetu, niwatake muendelee na kasi hii ya ukusanyaji wa mapato ya Serikali kwa kutumia Kituo cha Pamoja cha Huduma ambapo tayari kwa kipindi cha miezi mitatu ya mwanzo wa mwaka wa fedha wa 2018/2019, mwezi Julai hadi Septemba, 2018 mapato yameongezeka zaidi ya asilimia 100 kwa mwezi na kufikia asilimia 150”.

Naye Afisa Mfawidhi wa Forodha wa Kituo cha Huduma cha Pamoja cha Mtukula, Bwana Mohammed Shamte amesema kuwa katika mwaka wa fedha wa 2018/2019, malengo yao ni kukusanya kiasi cha shilingi bilioni 15.9 kwa mwaka ambapo tayari imeonekana kiwango hicho kitafikiwa kwa kuwa tayari kwa mwezi wanakusanya shilingi bilioni 1.3 ambazo ni wastani wa asilimia 110 hadi 150 ya makusanyo kwa mwezi ambayo yanavuka malengo. 

“Baada ya Serikali kuweka Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano, umeongeza spidi na uhakika wa kusafirisha taarifa na data tofauti na hapo awali tulipokuwa tunatumia satelaiti, hivyo Mkongo umewezesha ongezeko la mapato”, amesema Shamte.

Nditiye ameongeza kuwa Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano umebadilisha sekta ya mawasiliano nchini na kwenye nchi za jirani zilizounganishwa na Mkongo huo za Uganda, Rwanda, Burundi, Kenya na DRC Congo ambapo wanafurahia huduma za mawasiliano. 

“Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano lazima ulindwe, ni kama reli au barabara, na mawasiliano ni uchumi na maendeleo ambapo unaingiza mapato kwa Serikali yetu,” amesema Nditiye

Pia, amewataka wafanyakazi wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL Corporation) waendelee kuutunza na kuendesha Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano kwa kuwa ni watu sahihi, wana utaalamu na ujuzi wa kutosha kufanya kazi na Serikali imewaamini na kuwapa jukumu hilo kwa kuwa mawasiliano ni uchumi na ni usalama hivyo ukicheza na mawasiliano nchi inasambaratika.

Wakiwasilisha changamoto za mawasiliano kwa Nditiye, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Misenyi Bi. Thabitha Solomoni amesema kuwa wakati mwingine mtandao unakwenda taratibu au kukosekana hivyo kuathiri usafirishaji wa taarifa na data za watumishi kwa Serikali wa malipo na masuala ya watumishi

Naye Meneja wa TTCL Mkoa wa Kagera Bi. Irene Shayo amejibu changamoto hio kwa kusema kuwa inategemea aina ya kifurushi ambacho Halmashauri husika imenunua na wanachotumia. 

Ametoa rai kwa Halamshauri kutumia wataalamu wao kufahamu uwezo wa mtandao wa intaneti wanaotumia ili uweze kuendana na mahitaji na ukubwa wa taarifa au data wanazotuma au kupokea, hivyo Ofisi za Serikali zizingatie ubora wa huduma kuendana na mahitaji yao na TTCL ina ofisi zake nchi nzima, wako tayari kuwahudumia.

Nditiye amepokea changamoto hiyo kuhusu spidi ya intaneti kwenye ofisi zao na amewataka wataalamu wa TEHAMA  kupeleka mahitaji sahihi ya mtandao wa intaneti kwa Wakurugenzi wa Halmashauri zao na TTCL wako tayari kushauri ili mahitaji yanayotakiwa yaweze kutolewa na TTCL kuendana na mahitaji stahiki

Naye Mkurugenzi wa TEHAMA, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Bwana Mulembwa Munaku amewataka maafisa TEHAMA wote kufungia mitandao ya kijamii muda wa saa za kazi ili mtandao wa intaneti uweze kutumika vizuri kwa matumiz ya Serikali

Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Brigedia Jenerali Marco Gaguti amemweleza Nditiye kuwa bado hakuna mawasiliano ya kuridhisha kwenye maeneo mbali mbali ya mkoa huo licha ya kwamba makampuni yote ya mawasiliano yapo ila bado kuna changamoto ya upatikanaji wa mawasiliano ya uhakika kwenye mkoa huo

Akitoa ufafanuzi kuhusu changamoto hiyo, Nditiye amesema kuwa tayari Serikali imechukua hatua kuhusu jambo hilo kwa kuongeza minara ya mawasiliano kwenye maeneo ya mipakani ambapo mawasiliano ni hafifu kwa kuwaelekeza wataalamu wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote kufika kwenye maeneo hayo, kufanya tathmini na kupeleka mawasiliano kwa kuwa hadi sasa watanzania wanapata mawasiliano kwa kiwango cha asilimia 94 isipokuwa maeneo machache. 

Pia ameipa TTCL mwezi mmoja kuhakikisha vocha na laini za TTCL zinapatikana nchi nzima ili kuwawezesha watanzania kuwasiliana kwa kuwa mawasiliano ni uchumi na ni usalama

Nditiye amefanya ziara hiyo ya kukagua miundombinu ya Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano kwenye vituo vya mpakani vya Kabanga, Rusumo Mtukula na Biharamulo


from MPEKUZI

Comments