Waziri Lukuvi Kutatua Migogoro Ya Ardhi Ya Mikoa Nane Kwa Wiki Mbili

Na. Hassan Mabuye, Wizara ya Ardhi
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. William Lukuvi anataraji kufanya ziara ya kusikiliza migogoro na kero za wananchi zinanzohusu ardhi na kuzitafutia ufumbuzi katika mikoa nane ya Tanzania bara katika wiki mbili kuanzia tarehe 17 hadi 30 Septemba 2018.

Ziara hii ni katika utekelezaji wa kampeni yake ya “Funguka kwa Waziri wa Ardhi” ambayo aliizindua rasmi mwezi Januari mwaka 2018 yenye lengo la kuzunguka nchi nzima kusikiliza migogoro na kero za wananchi zinanzohusu ardhi na kuzitafutia ufumbuzi papo hapo.

Katika wiki mbili hizi za kutatua migogoro ya ardhi katika mikoa nane waziri Lukuvi ameeleza kuwa kuanzia tarehe 17 hadi 19 atakuwa katika mkoa wa Mara katika wilaya ya Bunda, Musoma na Tarime na baadae tarehe 20 hadi 30 atakuwa katika mikoa ya Tabora, Katavi, Rukwa, Songwe, Njombe, Iringa na Morogoro.

“Nipo njiani kuelekea mkoa wa Mara ambapo siku ya jumatatu tarehe 17 Septemba ntaanzia wilayani Bunda ili kutatua mgogoro wa Bibi Nyasasi Masike na kukagua kiwanja chake kama nilivyomuahidi Mheshimiwa Rais wakati alipofanya ziara yake wilayani Bunda na kunipigia simu moja kwa moja” Amesema Waziri Lukuvi.

Akaongeza Waziri Lukuvi, “nimeagizwa na Rais Magufuli katika kipindi cha miaka mitano hii hadi kufikia 2020 migogoro ya ardhi iwe imepungua kwa kiasi kikubwa kama sio kuisha na kazi hii ni utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM, na ninawaagiza viongozi wajitokeze kuwasikiliza na kutafutia ufumbuzi kero za wananchi wanyonge ambazo zimekuwa zikiwatesa kwa muda mrefu”

Aidha, ameongeza kuwa siku hiyo hiyo atasikiliza migogoro na kero za wananchi zinanzohusu sekta ya ardhi na kuzitafutia ufumbuzi katika mkutano wa hadhara uliyopo ukumbi wa Halmashauri ya wilaya ya Bunda.

Ameongeza kuwa baadae ataelekea wilaya ya Musoma na Tarime ambapo atasikiliza na kutatua kero za wananchi zinazohusu migogoro ya ardhi papo hapo pamoja na kusikiliza na kutatua kero ya ardhi ya Bibi Ghati Mwita Bukura na kuona eneo lake.

Baada ya ziara ya mkoa huo Waziri Lukuvi ataelekea mkoani Tabora na mkoani Katavi kutatua migogoro ya ardhi ya wakazi wa mikoa hiyo na kutatua migogoro ya matumizi ya ardhi kwa kufanya mikutano ya hadhara na wananchi kwa kutumia Kauli Mbiu ya Funguka kwa Waziri wa Ardhi na baadae kuelekea mkoani Rukwa.

Waziri Lukuvi katika Mkoa wa Rukwa anataraji kuutafutia ufumbuzi mgogoro wa ardhi wa Shamba la Malonje lililo na mgogoro wa muda mrefu pamoja na kusikiliza migogoro ya ardhi na baadae kuwasili mkoani Songwe wilayani Tunduma ambapo atakagua na kusikilisa changamoto za mpaka wa Tanzania na Zambia.

Ziara hiyo itaendelea katika mikoa ya Njombe na Iringa kutatua migogoro ya ardhi ya wakazi wa mikoa hiyo na kutatua migogoro ya matumizi ya ardhi kwa kufanya mikutano ya hadhara na wananchi kwa kutumia Kauli Mbiu ya Funguka kwa Waziri wa Ardhi na baadae kumalizikia katika mkoa wa Morogoro kwa ajili ya mgogoro wa eneo la Mabwegere

Waziri Lukuvi katika mwezi huu wa Septemba ameweza kutatua migogoro mikubwa katika mikoa ya Dar es salaam na Arusha katika nyakati tofauti, miongoni mwa migogoro hiyo ni ule wa mwekezaji wa kiwanda cha Minjingu na wananchi wa Pugu Stesheni jijini Dar es salaam ambao ameupatia ufumbuzi na wananchi wamefurahi kwa uamuzi wake.

Mgogoro mwingine alioupatia ufumbuzi ni ule wa eneo la msitu wa Kazimzumbwi ambao ulivamiwa na wananchi ambao walishindwa katika kesi na Waziri Lukuvi akatoa siku 30 ili kuwasaidia wananchi hao. Aidha mgogoro mwingine uliopatiwa ufumbuzi na Waziri Lukuvi akishirikiana na Waziri wa Mifugo na Uvuvi ni ule wa eneo la Pugu Mnadani ambalo pia wananchi wamevamia na limepatiwa ufumbuzi tayari.

Katika Mkoa wa Arusha Waziri Lukuvi ametembelea na kutatua migogoro mikubwa ya wakazi wa Wilaya ya Monduli katika vijiji vya Lolkisale, kijiji cha Lemooti, kijiji cha Eng’arooji, na Kijiji cha Nafco nyingine ni kata ya Sepeko, kata ya Mfereji iliyo na mgogoro kati ya Wilaya za Monduli na Arumeru ambapo ametatua kwa ufanisi mkubwa jambo ambalo limewafanya wakazi wa maeneo hayo kummwagia sifa na kumuombea kwa Mungu ampe umri mrefu wenye mafanikio.

Wizara inaendelea na utatuzi wa migogoro ya matumizi ya ardhi kwa kufanya mikutano na wananchi kwa kutumia Kauli Mbiu ya Funguka kwa Waziri wa Ardhi. Katika mikutano hiyo hadi sasa jumla ya malalamiko 4,168 yameshapokelewa na Wizara kwa kushirikiana na Halmashauri mbalimbali na imepatiwa ufumbuzi na mingine inaendelea kuchambuliwa ili kupatiwa ufumbuzi.


from MPEKUZI

Comments