Mabadiliko Madogo ya Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi Yaliyofanywa na Rais Magufuli

Rais John Magufuli leo tarehe 13 Agosti, 2018 amefanya mabadiliko madogo ya wakuu wa wilaya na wakurugenzi wa halmashauri mbalimbali nchini.

Uteuzi huo alioufanya Rais Magufuli umetangazwa leo Ikulu jijini Dar es Salaam na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi John Kijazi.

“Uteuzi huu umefanyika kufuatia mkuu wa wilaya ya Chato aliyeteuliwa hivi karibuni kwenda nje ya nchi kwa ajili ya mafunzo ya kijeshi, Kanali Patrick Norbert Songea,” amesema Balozi Kijazi.

Mabadiliko hayo ni pamoja na, uhamisho wa Mkuu wa Wilaya ya Kwimba, Msafiri Simion aliyehamishiwa wilayani Chato, wakati Senyi Ngaga akipelekwa Kwimba.

Kwa upande wa mabadiliko ya wakurugenzi wa halmashauri, Rais Magufuli ameteua wakurugenzi arobaini na moja (41) wapya na kuwahamisha wakurugenzi 19, akiwemo Dkt. Maulid Madeni aliyeteuliwa kuwa Mkurugenzi mpya wa Halmashauri ya Jiji la Arusha, huku Emanuel Mkongo akiteuliwa kuwa Mkurugenzi mpya wa Halmashauri ya Manispaa ya Meru.

“Rais Magufuli Amefanya uteuzi na uhamisho wa wakurugenzi wa halmashauri ya wilaya, miji,  manispaa na jiji, kwa kuteuwa wakurugenzi wapya 41 na kuhamisha vituo wakurugenzi 19. Mabadiliko haya ni kutokana  na wakurugenzi waliokuwa vituo hivyo kustaafu, kuhamishwa na  kupangiwa kazi nyingine na wengine kuondolewa kwenye nafasi za ukurugenzi.


“Wakurugenzi ambao katika mabadiliko haya wamebadilishwa vituo vya kazi, wanapaswa kwenda kuripoti katika vituo vyao vya kazi mara moja." amesema Balozi Kijazi na kuongeza;
 
“Kwa wale wakurugenzi walioteuliwa kwa mara ya kwanza wanatakiwa kuripoti kwa katibu mkuu wa Tamisemi siku ya Jumatano kwa ajili ya kiapo cha uadilifu na maelekezo ya majukumu yao.”

Balozi Kijazi amesema watakapokwenda Dodoma wanapaswa kuwa na vyeti vyao vya kidato cha nne, kidato cha sita na elimu ya taaluma.


from MPEKUZI

Comments