Lugola Aagiza Polisi Kuwakamata Waliofanya Ufisadi Sekta Ya Michezo

Na Felix Mwagara, MOHA
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola amemtaka Mkuu wa Polisi wa Wilaya ya Bunda kuwakamata watu walioshiriki kuwatapeli wananchi katika Sekta ya michezo wilayani humo, Mkoa wa Mara.

Watu hao ambao walitangaza kuanzisha ligi wilayani humo na kuzitaka timu za mpira wa miguu kata mbalimbali zichangie fedha na baadaye ligi hiyo haikufanyika na watu hao walikimbia na fedha hizo na kufanya wananchi hao waandamane wakitaka fedha zao zirudishwe.

Waziri Lugola akizungumza na mamia ya wananchi wa Mji wa Bunda baada ya kulizindua Bonanza la Amani wilayani humo, alisema kitendo walichokifanya watu hao ni ufiadi mkubwa hivyo lazima wakamatwe ili iwe funzo kwa wale wote wenye tabia ya kufanya ufisadi wa aina hiyo katika sekta ya michezo nchini.

“Nimeambiwa wanamichezo ambao walichangishwa waliandamana mpaka kwa Mkuu wa Wilaya kuelezea jinsi walivyoibiwa na watu hao, hata hivyo Mkuu wa Wilaya alitangaa watu hao warudishe fedha hizo, ila mimi nahitaji hawa watu wakamatwe haraka iwezekanavyo, huu ni ufisadi mkubwa na hakika Serikali hii ya awamu ya nne haitakubaliana na ufisadi huo.

Aliongeza kua, mahakama ya ufisadi inahitaji wateja hivyo waliofanya wizi huo pia ni mafisadi hivyo lazima wakamatwe haraka iwezekanavyo ili sheria ichukue mkondo wake.

Aidha, Bonanza ambalo alilizindua waziri huyo, linatarajiwa kufanyika nchini nzima limezinduliwa mjini humo na baadaye litafanyika nchi nzima likiwa na lengo kuu kutangaza amani nchini.

Waziri Lugola alisema, michezo inaleta amani michezo inaleta ushirikinao, michezo inaimarisha undugu, michezo inaimarisha ushikamano na michezo uepusha wananchi wasijiingize katika uhalifu, hivyo Wizara yake inatarajia Bonanza hilo litazidi kudumisha amani zaidi.

“Michezo ikiimarishwa tunaimarisha amani, tukishiriki michezo kama hivi wanaokuja kutazama na nyie mnaocheza,  hivyo muda mwingi tunautumia katika kufurahi pamoja na ndio mana vitendo vya uhalifu vitapungua kwasababu watu tunataka tuwe wamoja kupitia michezo,” alisema Lugola. 

Waziri Lugola aliongeza kua, Bonanza la kuhubiri amani sio kwamba linafanya wilyani Bunda bali litafnyika nchi nzima likiwa na lengo la kuwaweka watanzania pamoja ili amani nizidi kudumu.

“Hapa tulipo ni uwanja wa CCM na hii ilani ni ya CCM na katika ibara ya 160, 161 na 162 inazungumzia kuimarisha na kudumisha sekta ya michezo, hivyo tupo hapa kutokana na ilani hii ya CCM na lengo kuu ni kudumisha amani,” alisema Lugola.

Waziri Lugola yupo wilayani Bunda mkoani Mara kwa ajili ya ziara ya kutembelea miradi ya maendeleo ndany ya jimbo lake la Mwibara wilayani humo.


from MPEKUZI

Comments