Ajari ya Gari Ndogo na Lori Yaua Watu Wawili Babati

Watu wawili wamefariki dunia na mmoja kujeruhiwa baada lori la Halmashauri ya Wilaya ya Babati Mkoani, Manyara kuligonga kwa nyuma gari dogo eneo la Bashnet.

Kamanda wa polisi wa mkoa wa Manyara Kamishna Msaidizi (ACP) Augustino Senga amesema tukio hilo limelotokea Julai 17 saa 1 usiku eneo la Arry kata ya Bashnet barabara kuu ya Babati-Singida.

Akizungumza leo Julai 18, Kamanda Senga amesema chanzo cha ajali hiyo ni uzembe wa madereva wote wawili kwani  gari dogo  lilikuwa limeegeshwa bila kuweka alama yoyote na dereva wa lori hakuchukua tahadhari wakati anaendesha gari hilo la Halmashauri na hivyo kuligonga kwa nyuma.

Amesema dereva wa lori la Halmashauri hiyo Simon Mushi (56) alijeruhiwa na abiria wake Prosper Omera (25) na mwingine wa kike (20) ambaye hakufahamika jina lake walifariki dunia.

“Miili ya marehemu hao wawili imehifadhiwa kwenye hospitali ya mji wa Babati (Mrara) na majeruhi huyo anapata matibabu katika hospitali ya Dareda,” amesema

Amesema gari hilo dogo, lenye namba T 793 DTP aina ya Guhe likiwa limeegeshwa pembeni ya barabara, liligongwa kwa nyuma na dereva wa lori lenye namba SM 2541 aina ya Isuzu mali ya halmashauri ya wilaya ya Babati.

"Bado tunaendelea na uchunguzi wa tukio la ajali hiyo ambapo ni uzembe wa madereva wote wawili tunaendelea kuwatafuta mmiliki na dereva wa hilo gari lingine kwani hakukuwa na dereva wakati lilipokuwa limeegeshwa pembeni," alisema kamanda Senga.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Babati, Hamis Malinga amesema gari hilo lilipata ajali likiwa limetoka kupeleka vifaa vya mradi wa maji ikiwamo mabomba kwenye kijiji cha Ufana.

"Wale waliofariki walikuwa sehemu ya nyuma ya dereva waliminywa na kufariki dunia papo hapo ila dereva aliumia kidogo kichwani," amesema.


from MPEKUZI

Comments