Agizo La Waziri Jafo Kwa Wakuu Wa Mikoa Wote Nchini Ndani Ya Siku 60

 Angela Msimbira OR-TAMISEMI
 Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Seleman Jafo ametoa muda wa miezi miwili kwa Wakuu wa Mikoa wote nchini kuanza kusimamia ujenzi wa miundombinu ya shule katika Mikoa yao.

 Akizungumza na waandishi wa habari Ofisini kwake leo, Mhe. Jafo amesema miundombunu hiyo itahusisha ujenzi wa vyumba vya Madarasa 478 na mabweni 269 ambapo kila bweni moja litachukua wanafunzi 80.

 Mhe. Jafo alisema kuwa ni wajibu wa kila Mkuu wa Mkoa kusimamia kusimamia kwa dhati kazi ya ujenzi wa miundombinu ya Madarasa na Mabweni na kuhakikisha kuwa fedha zinazotolewa na Serikali zinaendana na majengo yatakayojengwa kama walivyokuwa wakifanya katika miradi ya afya na Elimu.

Aliendelea kusema kuwa Serikali imeweza kuchagua shule 119 ambazo orodha itatolewa wakuu wa Mikoa hiyo wahakikishe wanasimamia kwa haraka zoezi la kubaini maeneo ya yatakapojengwa madarasa na mabweni, pia kusimamia uteuzi wa Kamati za Ujenzi na kuanza mchakato wa kuwatafuta wajenzi wa majengo hayo.

 Alisema kuwa Serikali itatoa fedha kukamilisha haraka ujenzi wa miundombinu ya mabweni 269 na madarasa 478 kwa ajili ya wanafunzi kujiunga na Kidato cha Tano kwa kipindi hiki na kuagiza fedha hizo zikasimamiwe kwa weledi.

 Mhe Jafo alisema ujenzi wa miundombinu hiyo utatumika kwa njia ya “Force Accont” utaratibu unaotumika katika Mamlaka za Serikali za Mitaa na ambao umetuika katika ujenzi wa shule na vituo vya afya Nchini.

 Aliwaagiza Wakuu wa Mikoa wote ambao Halmashauri zao kazi ya Ujenzi wa Miundombinu ya Shule inaenda kufanyika kusimamia kwa nguvu mchakato wa kutafuta mafundi wa ujenzi wa majengo na kuhakikisha wanapatikana haraka ili kazi ianze mara moja baada ya kubainisha maeneo.

 Aliwataka Wakuu wa Mikoa kuhakikisha wamekamilisha ujenzi wa vyumba vya madarasa na mabweni ifikapo tarehe 30/8/2018 ili kuhakikisha wanafunzi walio na sifa ya kujiunga na kidato cha Tano watapata fursa ya kujiunga na kidato cha tano.

 Wakati huohuo aliwaagiza Wakurugenzi ambao watasuasua katika utekelezaji wa ujenzi wa miundombinu ya madarasa na mabwebi pamoja na miradi mingine hatasita kuwachukulia hatua na kuwataka watakapopata fedha wahakikishe kazi hiyo inakamilika mapema.

 “Niwatake Wakurugenzi ambao wanatabia ya kusuasua utekelezaji wa mradi mbalimbali kuacha mara moja na katika jambo hili sihitaji masiahara hata kidogo, Mamlaka za Serikali za Mitaa itakapo pokea fedha ihakikishe inakamilisha ujenzi huo haraka.” Alisema Jafo

 Aliendelea kusema kuwa Serikali haiwezi kukubali kuona watoto wa maskini wanakosa nafasi ya kujiunga na kidato cha Tano wakati wanasifa, hivyo amewataka nawata Wakuu wa Mikoa kusimamia kazi hiyo haraka kwa lengo la watanzania kuweza kupata fursa ya elimu katika nchi yao.

 Aidha alisema Serikali imetenga shilingi bilioni 29 kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu mbalimbali ikiwemo ya ujenzi wa vyumba vya madarasa ili kuhakikisha vijana wa Tanzania wanapata Elimu.


from MPEKUZI

Comments