Utafiti Twaweza: Wananchi 9 Kati Ya 10 wako tayari kulipia ada wakihakikishiwa elimu bora

Mitazamo ya wananchi kuhusu elimu bure imebadilika kwa kiasi kikubwa ndani ya miaka 12 iliyopita: mwaka 2005, zaidi ya nusu ya wananchi (56%) walisema kuwa ‘ni bora elimu itolewe bure kwa watoto wetu, hata kama kiwango cha elimu ni cha chini’.

 Mwaka 2017, wananchi 9 kati ya 10 (87%) wanasema ‘ni bora tukaongeza viwango vya elimu, hata kama itatulazimu kulipa ada.’ 

Wananchi 9 kati ya 10 (87%) wangependa serikali itumie fedha kwenye mpango wa kutoa mafunzo na kuwasaidia walimu kuliko kugawa sare za shule bure ikilenga kuwaondolea wazazi mzigo wa kununua sare hizo.

Matokeo haya yametolewa na Twaweza katika utafiti wake uitwao Elimu Bora au Bora Elimu? Elimu waitakayo watanzania. Matokeo ya muhtasari huu yanatokana na takwimu za utafiti wa Sauti za Wananchi, utafiti wa kwanza barani Afrika wenye uwakilishi wa kitaifa unaotumia simu za mikononi. 

Matokeo haya yanatokana na takwimu zilizokusanywa kutoka kwa wahojiwa 1,786 kutoka maeneo mbalimbali ya Tanzania Bara (Zanzibar haihusiki kwenye utafiti huu) kati ya mwezi Septemba na Oktoba 2017.

Utafiti huu umebaini kwamba ni wazazi wachache sana huzingatia ada nafuu (6%) na umbali wa shule (18%) wakati wa kuchagua shule za sekondari kwa ajili ya watoto wao. Badala yake wazazi wengi huzingatia zaidi viwango vya juu vya ufaulu wa shule husika (asilimia 72) na walimu wanaojituma (asilimia 72 pia). Wazazi wanataka elimu bora na wameonesha utayari wa kuigharamia.

Idadi ya kaya zinazowapeleka watoto wao kwenye shule za binafsi (asilimia 10) haijabadilika kati ya Agosti/Septemba mwaka 2016 na Septemba/Oktoba 2017. 

Hata hivyo, uandikishaji wa watoto kwenye shule binafsi hutofautiana kutoka na ngazi ya elimu, wazazi 3 kati ya 10 (27%) huchagua shule binafsi kwa ajili ya elimu ya awali na 2 kati ya 10 (17%) kwa ngazi ya sekondari ukilinganisha na mzazi mmoja kati ya kumi (7%) wanaoandikisha watoto wao kwenye shule za msingi za binafsi.

Hata hivyo, wazazi wanajitahidi kutekeleza majukumu yao: zaidi ya wazazi 5 kati ya 10 (53%) walichangia ujenzi wa shule mwaka uliopita; 4 kati ya 10 (38%) walitoa fedha, 1 kati ya 10 (18%) walichangia nguvu kazi na 1 kati ya 10 (9%) walitoa vifaa. 

Na kwa kawaida wazazi pia hulipia vifaa kama vile vya kuandikia (98%), sare za shule (75%), mabegi ya shule (26%) na vitabu (15%). Zaidi, 85% wanasema walikutana na walimu wa watoto wao angalau mara moja au mbili mwaka uliopita, ukilinganisha na 79% waliofanya hivyo mwaka 2016. Wazazi wengi zaidi (30%) wana uwezekano wa kukutana na walimu kila baada ya miezi michache ukilinganisha na mwaka 2016 (21%).

Zaidi ya nusu ya wazazi wnalipokea jukumu la msingi la kuhakikisha watoto wanajifunza japokuwa idadi kubwa kidogo (46%) pia wanasema jukumu hilo ni la walimu. 

Hakuna mzazi aliyesema jukumu la watoto kujifunza ni la maafisa elimu, wanasiasa au yeyote serikalini. Na pale walipouliuzwa ni kwa namna gani wanausaidia uongozi wa shule, wazazi wengi (52%) walizungumzia jukumu lao katika kuwaadhibu watoto wao na wengine wachache wakitaja ushiriki wao kwenye harambee za kuchangisha fedha (22%), kufuatilia mahudhurio ya walimu (14%) au kutoa maoni kwenye ukaguzi wa mahesabu ya shule (4%).

Mkurugenzi Mtendaji wa Twaweza, Aidan Eyakuze, anasema: “Ujumbe wa msingi wa wananchi kuhusu suala la elimu nchini ni huu: wako tayari kuilipia elimu bora kwa ajili ya watoto wao.

Mitazamo ya wananchi inaonekana kubadilika kwa kiasi kikubwa katika kipindi fulani, ikiashiria kuwa sasa wanaelewa kilichofanyika na walichopoteza. Utafiti huu unadhihirisha kuwa wananchi wanapaswa kuwa sehemu muhimu ya mjadala wa kitaifa utakaolenga kuboresha matokeo ya elimu yetu.”


from MPEKUZI

Comments