Maagizo Aliyoyatoa Rais Magufuli Kwa CCM

Baada ya muda mrefu kuwepo kwa vilio vya wapenda michezo nchini kote juu ya miundombinu mibovu ikiwemo viwanja, hatimaye Rais Magufuli ameliona hilo na kuagiza moja ya wamiliki wakubwa wa viwanja, Chama Cha Mapinduzi kuviboresha.

Akiongea jana kwenye hafla ya kukabidhi kombe kwa mabingwa wa ligi kuu soka Tanzania Bara, Rais Magufuli amesema wao kama serikali watashirikiana na TFF pamoja na vyama vingine vya michezo kuboresha miundombinu ili timu zifanye vizuri kimataifa.

''Niwaombe Chama Changu cha CCM ambao ndio wamiliki wa viwanja vingi nchini kuboresha miundombinu hiyo ili iwezeshe wanamichezo kufanya maandalizi mazuri yatakayofanikisha kufanya vizuri Afrika na duniani kimichezo'', alisema.

Kwa upande mwingine Waziri wa Habari, Dkt. Harrison Mwakyembe alimweleza Rais kuwa wao kama Wizara wanasubiri bajeti yao ya mwaka wa fedha 2018/19, ipitishwe Bungeni ili wafanye ukarabati wa viwanja vya Uhuru pamoja na Taifa kwaajili ya mashindano ya AFCON U17, 2019.

Ikumbukwe kuwa Tanzania itakuwa mwenyeji wa fainali hizo za mwakani kwa vijana wenye umri chini ya miaka 17. Tanzania itawakilishwa na Serengeti Boys ambayo mwaka 2017 ilishiriki nchini Gabon na kushika nafasi ya tatu.


from MPEKUZI

Comments