Wakili wa Abdul Nondo ( Mwenyekiti wa Mtandao wa Wanafunzi Tanzania (TSNP)) akwama polisi

Mwanasheria Jebra Kambole na Wakili wa Mwenyekiti wa Mtandao wa Wanafunzi Tanzania (TSNP), Abdul Nondo amefunguka na kusema kuwa mpaka sasa ameshindwa kuonana wala kuongea na mteja wake huyo ambaye anashikiliwa na jeshi la polisi.

Wakili huyo amesema kuwa amejaribu kufika ofisi ya Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) ili kujua hali ya mteja wake pamoja na kuweza kuongea naye lakini ameshindwa.

"Mpaka sasa sijafanikiwa kuzungumza wala kumuona kwa sababu mara ya mwisho wakati tunafanya mazunguzo na DCI ambaye ana mamlaka juu ya hilo kwa sababu Abdul Nondo alikuwa anashikiliwa ofisini kwake mpaka dakika ya mwisho, tulipokwenda ofisini kujaribu kumuona akasema sisi huyu mtu tunamshikilia kama kama mlalamikaji lakini siyo kama mtuhumiwa... kwa hiyo nyinyi kama Mawakili hamtakiwi kumhoji ila tukiona kwamba huyu mtu ni mtuhumiwa basi tutawaita muweze kuongea naye na kusikiliza maelezo yake.

"Sisi tulimweleza tunahitaji kumuona ili tuweze kujua afya yake ili tuweze kurejesha mrejesho kwa familia na Watanzania wengine kwa ujumla ambao wanahofia juu ya usalama wake akasema yupo salama" alisema Kombole

Aidha Wakili huyo aliendelea kudai kuwa mpaka sasa Abdul Nondo anashikiliwa kinyume na sheria kwa kuwa sheria ya makosa ya jinai haitoi ruhuusa kwa jeshi la polisi kumshikilia mlalamikaji.

"Anayeshikiliwa ni mtuhumiwa lakini mpaka siku ya leo hajaachiwa kama ni mtuhumiwa kweli kwa sababu mtu ambaye anakwenda kutoa taarifa polisi anaachiwa arudi nyumbani huwezi kushikiliwa huko polisi na kwa kuwa wao wanasema wanamshikilia ana haki ya kupata uwakilishi kwa sababu kwa mujibu wa sheria yetu ya mwenendo wa makosa ya jinai sura namba 20 ya sheria za Tanzania, kifungu cha tano kinasema kwa muda gani mtu atakuwa chini ya dola au polisi.

"Mtu ambaye amewekwa chini tu akiwa hana uhuru wa kwenda anakotaka huyo ina maana yupo chini ya ulinzi kwa hiyo kama upo chini ya ulinzi una haki ya kupata wakili kuweza kuongea naye na kujua nini kinaendelea na hatma yake na kupata fursa ya kuongea na ndugu zake na familia lakini fursa hiyo kwa Nondo haijapatikana kwani saizi ni muda mrefu  ameshikiliwa na jeshi la polisi" alisema Kombole

Mbali na hilo Wakili huyo amesema kuwa mpaka sasa wao hawajui Abdul Nondo ameshikiliwa kwa sababu zipi na kusema kuwa kijana huyo ameshikiliwa kinyume na sheria, kinyume cha Katiba, kinyume cha haki za binadam na kinyume na utaratibu wetu kama taifa kiujumla.


from MPEKUZI

Comments