Ujenzi wa reli ya kisasa Kutoa Ajira kwa Wananchi 600,000

Rais John Magufuli amesema ujenzi wa reli ya kisasa nchini utatoa ajira za moja kwa moja 30,000 na zisizo za moja kwa moja 600,000.

Akizungumza leo Jumatano Machi 14, 2018 wakati wa uzinduzi wa ujenzi wa reli hiyo kutoka Makutopora mkoani Dodoma hadi Morogoro, Rais Magufuli amesema mbali na kutoa ajira, ujenzi huo ukikamilika utanyanyua uchumi wa nchi.

“Ujenzi wa reli hii utasaidia kutunza barabara zetu kama mnavyojua nchi yetu imepinga hatua katika ujenzi wa barabara. Barabara zetu hazidumu kutokana na kubeba mizigo mizito ambayo inaweza kusafirishwa kwa njia ya reli,” amesema.

“Uwapo wa reli hii utapunguza gharama za ukarabati wa barabara zetu. Ujenzi wa reli hii utatoa ajira za moja kwa moja 30,000 na zisizo za moja kwa moja 600,000… juzi tuliambiwa sasa tumefikia watu milioni 55, watu wanasema kwa nini tunazaliana, mimi nasema tuazaliane tu. Mnapokuwa wengi mnakuwa na sauti. Katika jumuiya tulizopo sisi tupo wengi tuna sauti, jambo la msingi tuchape kazi,” amesema.

Amewataka Watanzania  kuacha kuogopa wingi wao na kwamba, jambo la muhimu ni kufanya kazi.

“Denmark ina watu milioni tano lakini wakati mwingine inatoa msaada hata kwa nchi kama Tanzania kwa sababu watu wake wanafanya kazi. Nchi nyingi duniani zimeshindwa duniani kwa sababu zinakopa halafu zinapewa masharti magumu. Sisi tumejenga kwa hela ndogo tofauti na ilivyotarajiwa,” amesema.


from MPEKUZI

Comments