TCRA, Mwakyembe Wamkabili Diamond

Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imesema kamati yake ya maudhui inafuatilia mahojiano ya mwanamuziki Nasseb Abdul maarufu Diamond aliyoyafanya katika kituo cha Redio cha Times jijini Dar es Salaam.

 Ofisa Mkuu Idara ya Utangazaji ya mamlaka hiyo, Andrew Kisaka amesema wamechukua uamuzi huo kwa kuwa mahojiano hayo yamefanyika katika kituo wanachokisimamia.

Katika mahojiano hayo, Diamond alimjibu Naibu Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Juliana Shonza kutokana na Serikali kuzifungia nyimbo 15 mwezi uliopita, zikiwemo mbili za mwanamuziki huyo.

Kisaka amefafanua kuwa kiutaratibu wao wanaangalia zaidi chombo ambacho wamekipa leseni na kwamba, masuala mengine yatashughulikiwa na mamlaka nyingine.

Amesema suala hilo kwa sasa linafanyiwa kazi na kamati ya maudhui na kuahidi kulitolea ufafanuzi siku za hivi karibuni akiwataka wananchi kuwa na subira.

Wakati TCRA ikisema hivyo, Waziri wa Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo, Dk Harrison Mwakyembe amesema amesikitishwa na matamshi ya Diamond kuhusu kufungiwa kwa nyimbo hizo aliyoyatoa katika kipindi hicho.
 
“Maamuzi ya kuzifungia baadhi ya nyimbo za wasanii wawili kwa kukiuka maadili yalifanywa kwa mujibu wa sheria na si kwa utashi binafsi wa Shonza ambaye analaumiwa na Diamond,” amesema.

“Diamond atambue kuwa Serikali ina taratibu zake na maamuzi ya naibu waziri ni ya wizara. Kama vikao na wasanii tumefanya vingi sana, lakini Diamond hakuwahi kuhudhuria vikao hivyo, si wajibu wa Serikali kumfanyia kikao cha peke yake.”

Amesisitiza, “Sheria ni ya watu wote bila kujali umaarufu au nafasi ya mtu katika jamii, hivyo msanii Diamond anapaswa kutii sheria na mamlaka zilizowekwa.”

Dk Mwakyembe ameeleza kuwa sio busara kwa Diamond  kushindana na Serikali na endapo ana ushauri wowote ni vyema akawasilisha kwa njia sahihi, lakini si kumshambulia naibu waziri kwa dharau na kejeli kama alivyofanya.

“Diamond kwa mafanikio aliyoyapata katika muziki, anatarajiwa kuwa mfano bora kwa wanamuziki wenzake. Napenda kuwakumbusha wasanii wote kwamba sanaa ni kazi kama zilivyo kazi nyingine,” amesema.

“Pamoja na kuwa na kipaji hicho, wasanii wanatakiwa kuzingatia sheria, kanuni na miongozo inayosimamia tasnia ya sanaa kama ilivyo kwa tasnia nyingine.”


from MPEKUZI

Comments