Polisi yamshikilia dereva tukio la mhasibu ubalozi Syria kujeruhiwa

Polisi Mkoa wa Kinondoni wanamshikilia mfanyakazi wa ubalozi wa Syria  nchini kwa tuhuma za kumjeruhi usoni mhasibu wa ubalozi huo,  Hassan Alfaouri na kumpora Euro 93,000 (Sh237milioni).

Akizungumza leo Jumatano Machi 21, 2018 kamanda wa polisi mkoani humo, Jumanne Muliro amesema tukio hilo lilitokea Machi 19, 2018 saa nane mchana eneo la Shule ya Msingi Oysterbay, jijini Dar es Salaam.

Amesema siku hiyo, mhasibu huyo akiwa katika gari na dereva wake wakielekea Benki ya Azania tawi la Mazdu House lililopo mtaa wa Samora wakipeleka fedha hizo, walipofika mtaa wa Zambia dereva huyo alianza kuendesha gari taratibu.

Amesema baada ya kupunguza mwendo, alisimama  na kuzima gari ghafla walitokea watu watatu; mmoja kati yao alikuwa na kipande cha nondo mkononi  na kuingia katika gari hilo na kumtaka mhasibu huyo awape fedha.

Muliro amebainisha kuwa uchunguzi wa awali unaonyesha kuwa tukio hilo lilipangwa na baadhi ya wafanyakazi wa ubalozi wasio waaminifu, akiwamo dereva huyo ambaye wakati uporaji ukiendelea, hakutoa msaada wowote.

"Walivyoona anakawia kutoa fedha walimjeruhi usoni kwa kipande cha nondo, walimshusha dereva kwa nguvu na kuondoka na gari hilo,” amesema.

Amesema baada ya tukio hilo, polisi walianza msako  na kuikuta gari hiyo ikiwa imetelekezwa Msasani Bonde la Mpunga.


from MPEKUZI

Comments