Masauni Ajitosa Sakata la Maandamano Nchi Nzima

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamad Masauni amejitosa sakata maandamano linalosambaa katika mitandao ya kijamii, kwa kuwaonya wanaotishia kuandamana kwa kusema kuwa vyombo vya ulinzi na usalama viko imara.

Masauni ametoa kauli hiyo leo Alhamisi Machi 15, jijini Dar es Salaam wakati akipokea vituo sita vya polisi vinavyohamishika vilivyotolewa na kampuni ya vinywaji baridi ya Coca-Cola kwa Jeshi la Polisi Mkoa wa Kipolisi Kinondoni.

“Kuna watu wako ndani ya nchi na wengine nje ya nchi wanaotaka kukwamisha ajenda ya maendeleo watupeleke kwenye ajenda zisizo za msingi.

“Utasikia mwingine anasingizia polisi kuwa katekwa kumbe kajiteka mwenyewe, mwingine anataka watu waandamane, yaani watu waache kutumia fursa zilizopo kwa mfano jana Rais kazindua reli ya umeme ambayo mimi nilikuwa naiona Ulaya leo inajengwa Tanzania, waache  kutumia fursa za viwanda vinavyoibuka kwa wingi kama uyoga eti wakaandamane.

“Ninachoweza kuwahahikikishia ni kwamba vyombo vyetu viko imara,” amesema Masauni.


from MPEKUZI

Comments