DSE yafafanua kuhusu kupungua kwa mauzo ya hisa

Kufuatia baadhi ya watu katika mitandao ya kijamii kuhusisha upunguaji wa mauzo ya Soko la Hisa la Dar es Salaam-DSE na hali ya uchumi, Afisa Mtendaji Mkuu wa Soko hilo Moremi Marwa ametoa ufafanuzi wa muenendo wa soko hilo.

Amesema kupungua huko ni hali ya kawaida katika soko kunakotokana na wawekezaji kupendelea kubadili uwekezaji kutoka kwenye hisa kwenda kwenye hati fungani, na kwamba hali hiyo ikitokea mauzo ya hisa hushuka wakati ya hati fungani yakipanda.

Huku akirejea takwimu zinazoonyesha mwenendo wa soko katika kipindi cha robo mwaka wa 2017 na 2018, amesema kuanzia Januari hadi Machi 10 mwaka huu kulikuwa na miamala ya mauzo ya hisa zenye thamani ya jumla ya Sh. bilioni 72 na mauzo ya hati fungani-Bonds yalikuwa na thamani ya bilioni 287 kwa bei ya kuuzia.

Ukilinganisha na kipindi cha robo mwaka cha 2017 ambapo kulikuwa na miamala yenye thamani ya sh. 75 na thamani ya bonds ilikuwa bilioni 229, na kwamba mwaka huu mauzo ya bonds yalipanda kwa bilioni 58 hali iliyopelekea kushuka kwa mauzo ya hisa.

“Tunaweza kusema mwenendo ni kuwa wawekezaji wana hama kati ya hisa na hati fungani, hii ni hulka ya kawaida ya soko na wawekezaji, pia viashiria vingine kama market capitalization na indices karibu zote zinapanda ukilinganisha na mwaka uliopia,” amefafanua.

Ameongeza kuwa, “Mlinganisho wa kila wiki hasa ukizingatia kwa muktadha wa maendeleo na uchanga wa soko letu na mauzo kwa vipindi vya muda mfupi kama vile siku au wiki haielezi upana na uhalisia wa mwenendo wa soko.”


from MPEKUZI

Comments