Waziri Mkuu: Watumishi Na Madiwani Shirikianeni

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka watumishi wa Halmashauri na Mji wa Bunda pamoja na Madiwani washirikiane katika utekelezaji wa ujenzi wa miradi ya maendeleo.

Pia amewaagiza watumishi wa umma katika halmashauri ya wilaya na mji wa Bunda wafanye kazi kwa bidii na wawahudumie wananchi bila ya ubaguzi wa aina yoyote.

Waziri Mkuu aliyasema hayo jana (Ijumaa, Januari 19, 2018) wakati akizungumza na watumishi na Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya na wa Halmashauri Mji wa Bunda, katika ukumbi wa Halmashauri ya Bunda.

“Watumishi wa umma  acheni kukaa sana maofisini tengeni muda wa kuwatembelea wananchi katika maeneo yao na shirikianneni nao katika kutatua kero zinazowakabili. Madiwani na watumishi lazima mshirikiane ili kuwaletea wananchi maendeleo.

Alisema watumishi na madiwani wakishirikiana katika usimamizi wa utekelezaji wa miradi mbalimbali  ya maendeleo, wilaya itafanikiwa katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Pia Waziri Mkuu aliwasisitiza watumishi hao kufanya kazi kwa mujibu wa sheria na taratibu za utumishi  na wajiepushe na vitendo vya rushwa, wizi , ufisadi na uzembe kwa sababu vinarudisha nyuma maendeleo ya wananchi.

Awali, Waziri Mkuu alikagua mradi wa maji wa Bunda na baadae alizindua kikundi cha Ushirika cha Igembe Sabo na kukagua skimu ya umwagiliaji wa zao la mpunga ya Nyatwali wilayani Bunda.

Waziri Mkuu alihitimisha ziara yake wilayani Bunda kwa kuhutubia mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa Stendi Mpya katika mji mdogo wa Bunda.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU


from MPEKUZI

Comments