Sumaye asema kuzuiwa mikutano ya hadhara ni uonevu kwa wananchi

Waziri Mkuu wa mstaafu, Frederick Sumaye amesema zuio la kufanya mikutano ya hadhara hadi mwaka 2020, linaminya uhuru wa wananchi wenye nia ya kuanzisha vyama vipya ya siasa.

Sumaye ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chadema Kanda ya Pwani na Mjumbe wa Kamati Kuu ya chama hicho kikuu cha upinzani nchini ametoa kauli hiyo jana Januari 14, 2018 katika mahojiano na kituo cha Televisheni cha Azam.

Amesema zuio la kufanya mikutano liko kinyume na sheria iliyoanzisha vyama vya siasa.

“Jambo jingine ambalo ni gumu zaidi, nikisema leo si mwana CCM sitaki kwenda CCM, CUF wala Chadema, kwa utaratibu ulipo sasa siwezi kuanzisha chama kwani huwezi kufanya mkutano wowote kwa sababu tunafunga kabisa mtu kuanzisha chama,” amesema Sumaye na kuongeza,

 “…, CCM wao wanaonekana hawana wa kuwazuia, Mwenyekiti wao (Rais John Magufuli) anakwenda popote, wakati wowote ingawa unashindwa kumtofautisha na ziara za kiserikali.”

Kuhusu hamahama ya wanachama amesema, “ “Wanacheza na fedha za wananchi,  mfano mbunge wa Kinondoni (Maulid Mtulia aliyehamia CCM) alikuwa CUF, anakwenda CCM halafu wanamrudisha tena kugombea.”

“Sawa na yule wa Siha (Dk Godwin Mollel amehamia CCM) naye karejeshwa kugombea. Hii ni sawa na kuwatukana watu.”


from MPEKUZI

Comments