Juma Nkamia Azidi Kukomaa Muda wa Urais Uongezwe Hadi Miaka 7

Mbunge wa Chemba kwa tiketi ya CCM, Juma Nkamia amefunguka na kusema amemsikia Rais kuhusu kutohitaji kufanya mabadiliko ya Katiba na kubadili ukomo wa Urais na kudai Rais mwenyewe hawezi kusema anataka kuendelea kuongoza bali watu ndiyo hupelekea hilo.

Juma Nkamia amesema hayo wakati akiongea na kituo kimoja cha habari cha Kimataifa na kudai kuwa ametafakari kauli ya Rais Magufuli na kuomba ushauri kutoka kwa watu na mwisho kusema kuwa yeye haoni tatizo Rais kubadili ukomo wa Rais kutoka miaka 5 mpaka 7 hivyo atazungumza na Spika wa Bunge Mhe. Job Ndugai

"Mhe. Rais ambaye ni Mwenyekiti wa chama changu amesema yeye asingependa na hafurahishwi na hilo jambo sasa mkubwa akishasema wewe uliopo chini unatafakari hoja yako kwanza na unapata ushauri pia lakini mimi nakubaliana na hoja yake. Ila siyo yeye anayetaka kuendelea, mimi kwa mtazamo wangu na kwa kazi anazofanya na nikipita katika maeneo mengi wananchi wanaridhika na utendaji wake na siku zote haiwezekani Rais mwenyewe akasema mimi nataka kuendelea, bali ni wale ambao tunamuangalia utendaji wake wa kazi ndiyo wanaweza kutoa mapendekezo" alisema Nkamia

Mbunge huyo alizidi kusisitiza kuwa "Mimi niseme kwamba sisi wananchi pamoja na mimi na nafasi yangu kama Mbunge na kwa mujibu wa Kanuni na taratibu za Bunge ninaona kwamba Mhe. Rais kubadilisha miaka mitano kwenda saba si jambo la ajabu sana. Hivyo kwa mujibu wa kanuni za Bunge nitazungumza na Mhe. Spika na maelekezo ambayo nitapewa na Spika wa Bunge nitayafanyia kazi" alisema Nkamia

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli mnamo tarehe 13 Januari, 2018 alifunguka na kuweka wazi kuwa haridhishwi na hapendi mjadala uliokuwa ukiendelea kuhusu kufanya mabadiliko ya Katiba na kuongeza ukomo wa uongozi kutoka miaka mitano ya sasa na kwenda miaka saba.


from MPEKUZI

Comments