Benki Yaamua Kuuza Shamba Lake Kujinasua kufungiwa na Benki Kuu (BoT)

Chama Kikuu cha Ushirika mkoani Kilimanjaro (KNCU), kimejitwisha jukumu la kuinusuru Benki ya Ushirika ya KCBL isinyang'anywe leseni na kufungiwa na Benki Kuu (BoT), kwa kuamua kuuza ekari 581 za Shamba la Lerongo.

KCBL inakabiliwa na upungufu wa mtaji, tatizo ambalo hualika BoT kunyang'anya leseni na kufungia benki husika, ikiwamo tano kwa pamoja mwanzoni mwa mwezi huu.

Aidha, benki hiyo ambayo inamilikiwa na KNCU kwa asilimia 69, inahitaji kiasi cha Sh. bilioni tano ili kufikisha mtaji wa Sh. bilioni 6.5 ulioelekezwa na BoT uwe umefikiwa hadi ifikapo Juni, mwaka huu.

Uamuzi wa kuuza shamba hilo ulitangazwa jana na Mwenyekiti wa KNCU, Aloyce Kitau, wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mkakati wa kuinusuru benki hiyo isifutiwe leseni.

“Baada ya kupokea taarifa juu ya upungufu wa mtaji wa kuendesha benki yetu ya ushirika, wanachama wa KNCU (1984) Ltd, waliridhia kuuza moja ya mali zake na fedha itakayopatikana iongezwe kwenye mtaji wa benki hiyo ili ifikie kiasi hitajika cha mtaji kama ilivyoelekezwa na Benki Kuu,” alisema Kitau.

Shamba la Lerongo lililowekwa sokoni kwa sasa na ambalo bado zabuni yake haijatangazwa hata hivyo, lipo katika wilaya ya Siha.

Kitau aliwasihi wananchi wa mkoa wa Kilimanjaro kuendelea kutumia benki hiyo kwani hadi kufikia jana michakato yote na kibali cha kuuza shamba hilo ilikua imekamilika, na kwamba KCBL itafikia mtaji husika kama inavyotakiwa kisheria mapema iwezekanavyo.

Wakati huo huo, taarifa iliyotolewa kwa umma jana na makamu mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Benki ya KCBL, Tumaini Yarumba ilisema benki hiyo itatimiza vigezo vyote vya kuwa na mtaji hitajika kufikia Juni.Kwa mujibu wa Yarumba, Benki Kuu iliitaka KCBL kuhakikisha inaendelea kutoa huduma kwa wananchi wote wa mkoa wa Kilimanjaro.

Taarifa hiyo inakwenda sambamba na tangazo la BoT la Januari 9, mwaka huu linalotaka wananchi kuwa na imani kwa sekta ya kibenki nchini kuwa iko imara na tayari kuwahudumia Watanzania wote kwa ukaribu.

Akitoa ufafanuzi kuhusu umiliki wa benki hiyo, Meneja wa KCBL, Joseph Kingazi alisema benki hiyo ya ushirika ina wanahisa 245 ambao ni Vyama vya Ushirika wa Mazao (Amcos), Vyama vya Ushirika vya Akiba na Mikopo (Saccos) pamoja na watu binafsi.

KCBL iliyoanzishwa miaka 20 iliyopita, ndiyo benki ya kwanza ya ushirika nchini kufunguliwa na Rais mstaafu wa awamu ya tatu, Benjamin Mkapa na ndio waanzilishi wa mfumo wa stakabadhi ghalani.



from MPEKUZI

Comments