Rais Magufuli Alitaka Jeshi La Magereza Kujitathimini

Na Mwandishi Wetu,MAELEZO
RAIS Dkt. John Magufuli amelitaka Jeshi la Magereza Nchini kutathimini utendaji kazi wake kutokana na mwenendo usioridhisha wa jeshi hilo katika kutekeleza miradi mbalimbali inayopewa na Serikali.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa Nyumba za Makazi ya Maafisa na Askari wa Jeshi hilo, leo (Alhamisi Januari 23, 2020) Ukonga Jijini Dar es Salaam, Rais Magufuli alisema ameshangazwa na kasi isiyoridhisha ya utekelezaji wa miradi katika jeshi hilo licha ya kuwa na ukubwa wa kambi 129 nchini.

Akitolea mfano Rais Magufuli alisema Jeshi la Magereza lina jumla ya kambi 129 huku Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) likiwa na kambi 24 tu, lakini ameshangazwa na Magereza kujengewa nyumba za askari wake na JKT huku akishindwa kutumia nguvu kazi ya wafungwa walionao katika magereza mbalimbali nchini.

‘’Baada ya kutoa msamaha wa wafungwa zaidi ya 5000, sasa hivi katika magereza yote nchini kuna zaidi ya wafungwa 13,000 lakini tunashindwa kujenga nyumba za askari wetu, udongo kutoka kwa mungu tunao, hamna budi kujipanga na kuweka mikakati ili kuimarisha makazi ya askari ambao wanateseka’’ alisema Rais Magufuli.

Alisema mwezi Machi 2016 Serikali ilitoa kiasi cha Tsh Bilioni 10 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za askari magereza katika eneo la Ukonga Jijini Dar es Salaam na kutoa zabuni hiyo kwa Jeshi hilo pamoja na Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), ambapo pamoja  kutumia miezi 27  walishindwa kuikamilisha kazi hiyo kwa kufikia asimilia 40-45 ya ujenzi wake.

Akifafanua zaidi alisema kutokana na kutoridhishwa na kasi hiyo, Serikali iliamua kuipa zabuni ya ujenzi wa mradi huo huo, Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) ambapo ndani ya kipindi cha miezi 6 kuanzia mwezi Machi hadi Desemba mwaka 2019 ilikamilisha asilimia 55 ya ujenzi mradi huo kwa kutumia kiasi cha Tsh Bilioni 3 na kufanya mradi wote kutumia Tsh Bilioni 13.

Alibainisha kuwa ipo baadhi ya miradi mikubwa inayosuasua kutekelezwa na Jeshi hilo, ikiwemo Mradi wa Ujenzi wa Kiwanda cha Viatu katika Gereza la Karanga unaojengwa kwa ubia baina ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) na Jeshi la Magereza Nchini, ambao hadi sasa ujenzi wake hauridhishi kwani hakuna hata jengo moja lililokamilika hadi sasa.

‘’Mashine za kiwanda kile tayari zimewasili katika Bandari ya Dar es Salaam, lakini hadi sasa ni jengo moja tu lililofikia asilimia 49 ya ujenzi ndilo limesimama, sasa hizo mashine zitaenda kufungwa wapi, Mkataba wa Bilioni 9 umesainiwa, na ni mradi wenye ubia, kwa nini tunakwama’’ alisema Rais Magufuli.

Aidha Rais Magufuli aliipongeza JKT kutokana na kazi kubwa na nzuri inayofanya katika kusimamia na kutekeleza miradi mikubwa nchini ikiwemo ujenzi wa ukuta wa Mererani, Ujenzi wa Mji wa Serikali Dodoma na Ukuta wa Ikulu Dodoma wenye urefu wa Kilometa 27, na kulitaka Jeshi la Magereza kuiga mfano huo katika kujenga na kuboresha nyumba za makazi ya askari wa Jeshi hilo.

Kwa upande wake, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dkt. Hussein Mwinyi alisema Wizara yake inatambua juhudi kubwa zinazofanywa Rais Dkt. John Magufuli katika kuimarisha na kuboresha maslahi ya Maafisa na Askari wa Majeshi ya Vikosi vya Ulinzi na Usalama nchini ikiwemo ujenzi wa nyumba za makazi ya askari.

Waziri Mwinyi alisema katika Makazi hayo, yenye jumla ya ghorofa 12 zikiwemo ghorofa 8 za makazi askari na ghorofa 4 za makazi ya maafisa, zina jumla ya nyumba 172 zenye uwezo wa kutunza familia za maafisa na askari wa vikosi vya majeshi ya ulinzi na usalama.




from MPEKUZI

Comments