Kabudi: Niliandika Barua Ya Kujiuzulu Baada ya Mchakato Kuwa Mgumu, Lakini Ilichanwa

Rais Magufuli leo ameshuhudia utiaji saini wa makubaliano kati ya Serikali ya Tanzania na Kampuni ya madini ya Barrick.

Kabla ya utiwaji wa saini Waziri wa Mambo ya Nje nchini Tanzania, Profesa Palamagamba Kabudi  amezungumzia namna mchakato ulivyokuwa na changamoto.

Kabudi anasema alichukua uamuzi wa kuandika barua ya kujiuzulu  baada ya mchakato wa majadiliano na wajumbe wa Barrick kuwa magumu, kwamba aliona aibu kushindwa kazi aliyotumwa.

“Wakati wa mchakato wa makubaliano na Kampuni ya Barrick, nilisumbuliwa sana kule Canada ikafika wakati nikakata tamaa, nikasema sijawahi kutumwa kazi na Mkuu wangu na nikashindwa nikaandika barua ya kujiuzulu, wengine wakanipokonya wakaichana“ - Amesema Waziri Kabudi


Amesema wakati huo alikuwa katika wakati mgumu kwani Rais  Magufuli alikuwa akiuliza mambo yanayoendelea, huku bungeni wabunge wakihoji majadiliano ambayo wakati huo hayakuwa yakienda vizuri.

“Kuna wakati walikuja Wachina tofauti wa kuwekeza tukaongea nao ila wakaingia mitini, huku bungeni unapigwa mijeledi, huku Wachina wale wameingia mitini, huku Rais anasubiri umalize, huku unajiuliza utatoka kwa aibu ila Mungu akasimama na sisi,” amesema Profesa Kabudi.


Waziri huyo ameomba radhi kwa lolote litakalopungua, akibainisha kuwa utakuwa upungufu wa kibinadamu


“Tumeanzisha Kampuni ya Twiga, hatuna Barrick pekee Tanzania, tuna Barrick na Serikali ya Tanzania ndani ya Twiga

“Wakati wa majadiliano kati ya Tanzania na Barrick Prof. John Thornton alikubali mikataba haikuwa mizuri na lazima irekebishwe, na Rais Magufuli alisema sitaki mikataba irekebishwe kwa ajili yangu, fedha yote itakayopatikana itakwenda kwenye shule, afya, miundombinu nk"


from MPEKUZI

Comments