Bodi ya Manunuzi na Ugavi Yaagizwa Kuwachukulia Hatua Wanunuzi Waliokwenda Kinyume Na Maadili

Na Peter Haule na Josephine Majura, WFM, Dodoma
Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Ashatu Kijaji, ameiagiza Bodi ya Manunuzi na Ugavi kuwachukulia hatua waliopelekwa kwenye baraza la maadili  kulingana na uzito wa makosa yao ili taaluma hiyo iendelee kufanya kazi kwa weledi bila rushwa.

Agizo hilo limetolewa Jijini Dodoma wakati wa mkutano wa 10 wa Wataalamu wa Ununuzi  na ugavi kutoka maeneo mbalibali nchini.

Dkt. Kijaji alisema kuwa, kuna ununuzi usiozingatia sheria na kanuni na kusababisha kununua bidhaa zilizo chini ya kiwango, ununuzi hewa wa huduma na bidhaa na kutokuwepo kwa kumbukumbu za ununuzi na mikataba hewa licha ya uwepo wa wataalam hao.

“Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi wa Umma kwa mwaka 2018/19 inaonesha mikataba 12 kutoka taasisi tisa za umma yenye thamani ya shilingi bilioni 25.8 ina viashiria vya rushwa kwa kuwa utaratibu wa manunuzi kwa mikataba hiyo haukufuatwa”, alieleza Dkt. Kijaji

Alisema kuwa taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali inaonesha kuwa ununuzi wa jumla ya Sh. bilioni 16.6 haukuwa kwenye bajeti wala mpango wa ununuzi ulioidhinishwa na Sh. bilioni 24.85 zimetumika kulipa mikataba ambayo haikuwa na hati ya utekelezaji.

Dkt. Kijaji amewataka waajiri wote kutoa ushirikiano kwa bodi za kitaaluma hususan linapojitokeza suala la usimamizi wa maadili kwa wataalamu waliosajiliwa na bodi husika, kwa kuwa hakuna ufanisi bila maadili.

Aidha Dkt. Kijaji, ameupongeza uongozi wa PSPTB kwa hatua zilizochukuliwa za kusimamia mahitaji ya ajira ya kada ya ununuzi na ugavi kwa kuwapeleka mahakamani watu wanaofanya kazi za ununuzi na ugavi bila kuwa na sifa stahiki.

Hivyo akawataka waajiri wote kuhakikisha wanaajiri watumishi wenye sifa zinazotambuliwa na PSPTB na kuzingatia mahitaji yaliyopo kwenye waraka wa Maendeleo ya utumishi wa mwaka 2015.

Naibu Waziri Dkt. Ashatu Kijaji, ameiagiza Bodi ya Wataalamu wa Ununuzi na Ugavi (PSPTB) kufanya tathmini ya uwezo na uadilifu wa taasisi za umma zilizobeba dhamana ya ununuzi Serikalini.

Alielekeza kuwa taarifa ya Baraza la Maadili iwasilishwe wizarani mapema ili iweze kupitiwa na kufanya maamuzi kwa kushirikiana na vyombo vingine vya Serikali.

Amesema kuwa Wizara ya Fedha na Mipango itaendelea kuunga mkono juhudi za Bodi zinazolenga kuondoa kabisa uzembe na ukiukwaji wa maadili katika fani ya ununuzi na ugavi, kwa kuwa bajeti ya ununuzi wa Serikali ni takribani asilimia 80 ya bajeti yote.

Kwa upande wake Kamishna wa Idara ya Sera ya Ununuzi wa Umma, Dkt. Fredrick Mwakimbinga, alisema kuwa Bodi inafanya jitihada za dhati kuhakikisha taaluma ya ununuzi na ugavi inatoa mchango unaotarajiwa katika ujenzi wa uchumi wa viwanda kulingana na malengo ya Serikali ya Awamu ya Tano, ili kutimiza malengo hayo bodi imetoa mafunzo mahususi kwa taasisi mbalimbali ambayo yameongeza ufanisi katika taasisi husika.

Naye Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa PSPTB, Bw. Godfrey Mbanyi, amesema kuwa Bodi hiyo imeahidi kufanyia kazi maagizo yote yaliyotolewa na Naibu Waziri Dkt. Kijaji. Amebainisha kuwa licha ya kuwa na Sheria inayowataka watumishi wanaofanya kazi ya ununuzi na ugavi kusajiliwa, bado wapo ambao hawafanyi hivyo, Bodi itaendelea kuchukua hatua stahiki kwa wale wote watakao kiuka sheria.

Mwisho.


from MPEKUZI

Comments