Wadau Waliomba Bunge Kuridhia Itifaki Ya Mitandao Ya Tehama

Na Prisca Ulomi, WUUM
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isack Kamwelwe amewasilisha Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Mitandao ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (EAC Protocol on ICT Networks) kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu ili waweze kuipitia na kuridhia kabla ya kuiwasilisha kwenye Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Baada ya Kamwelwe kuwasilisha Itifaki hiyo mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu chini ya Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Selemani Kakoso, Kamati ilipokea Itifaki hiyo na kualika wadau wa Sekta ya Mawasiliano ili waweze kufika mbele ya Kamati hiyo na kutoa maoni yao.

Kamwelwe aliwaeleza wajumbe wa Kamati hiyo kuwa madhumuni ya Itifaki hiyo ni kuendeleza uunganishaji wa miundombinu ya TEHAMA mipakani; kuwezesha matumizi ya pamoja ya miundombinu ya TEHAMA, ikiwa pamoja na masafa na namba; kuwezesha matumizi ya huduma za mitandao ya TEHAMA bila upendeleo; kuendeleza matumizi ya huduma za mitandao ya TEHAMA Serikalini na kwenye sekta binafsi ikijumuisha Serikali Mtandao, Biashara Mtandao, mfumo wa “Geospatial Information.

System (GIS)” na utangazaji; kuwianisha sera, sheria na programu za TEHAMA
zitakazowezesha kufikiwa kwa malengo ya itifaki; kutoa elimu bora na mafunzo
yanayohitajika kwa ajili ya uongozi wa kimkakati, usimamizi, utafiti na ujuzi katika eneo la mitandao ya TEHAMA ndani ya Jumuiya; kuendeleza mashirikiano baina ya sekta ya umma na binafsi; kuwezesha upatikanaji wa mawasiliano kwa wote hususan kuunganisha visiwa na nchi zisizopakana na bahari; na kuhakikisha usalama na ubora wa huduma za mawasiliano na kuwezesha matumizi salama ya mtandao.

Aliongeza kuwa kwa upande wa Tanzania, nchi yetu imejiimarisha kwa kuweka
miundombinu muhimu ya TEHAMA ambayo ni pamoja na Mkongo wa Taifa wa
Mawasiliano ambao umejengwa na kufika katika Mikoa 26 ya Tanzania Bara pamoja na Zanzibar na kufikisha kwenye maeneo tisa ya mipaka na nchi jirani ikiwemo Kenya, Rwanda, Burundi na Uganda ambapo kuna watoa huduma za mawasiliano wa nchi hizo wanaotumia Mkongo wa Taifa. Pia, nchi za Rwanda, Uganda, Zambia na Malawi zinategemea uwepo wa miundombinu ya TEHAMA ya Tanzania kuwasiliana kimataifa.

Vilevile, watoa huduma wa nchini Kenya wanatumia Mkongo wa Taifa wa Tanzania kupitisha mawasiliano yake kwenda nchi nyingine. Miundombinu mingine iliyopo ni Kituo cha Taifa cha Kuhifadhi Data, Vituo sita vya maunganisho ya watoa huduma za intaneti (Internet Exchange Point – IXPs), miundombinu ya utangazaji pamoja na Mfumo wa Kuratibu na Kusimamia Mawasiliano (Telecommunication Traffic Monitoring System-TTMS). Pia, Serikali inaendalea kukamilisha Mkakati wa Taifa wa Mtandao wa
Kasi (National Broadband Strategy).

Wakitoa maoni yao kuhusu Itifaki hiyo mbele ya wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, wadau mbali mbali wakiwemo Kampuni ya Simu ya Airtel, Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL), Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) na Kituo cha Taifa cha Kuhifadhi Data (NIDC) wameridhia Itifaki hiyo na kuomba Bunge kupitia Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu iliridhie na kupitisha Itifaki hiyo Meneja wa Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano, Adin Mgendi alisema kuwa, “Itifaki hii nimekuja wakati muafaka, Tanzania imekuwa mdau wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, imejenga miundombinu na kuwezesha nchi za jirani zisizopakana na bahari kupata
mawasiliano.

Itifaki hii itatuweka mahali pazuri na tutashirikiana vema, kwa sasa
tunaingia makubaliano baina ya nchi mbili na kupeleka mawasiliano, ila tukitofautiana hakuna pa kwenda, ila kupitia itifaki hii tutaendelea kufungua masoko EAC na nchi za SADC ambapo hadi sasa tumeunga Malawi na tunaendelea Msumbiji,”.

Naye Mkuu wa Kitengo cha Usimamizi na Utekelezaji wa TCRA, Dkt. Phillip
Filikunjombe alisema kuwa Itifaki hii ikipitishwa, nchi wanachama wa EAC tutakuwa na fursa ya kukaa pamoja na kuja na sheria zinazofanana na zinazoendana na matakwa ya nchi yetu katika kudhibiti uhalifu mtandaoni

Filikunjombe alifafanua kuwa Tanzania tumefunga mtambo wa TTMS ambapo Itifaki hii inazungumzia mifumo ya kudhibiti usalama wa mtandao kwa kuwa Tanzania sio kisiwa na uhalifu mtandao hauna mipaka, tutahakikisha nchi za wenzetu wanakuwa na mifumo yenye viwango vinavyohitajika kudhibiti usalama kwa kuwa hawana mfumo kama TTMS hivyo tutahakikisha nao wanafunga mifumo ya kudhibiti uhalifu wa mtandao na usalama.

Mwakilishi wa Airtel, Delfina Martin alisema kuwa kampuni yao imeridhia Itifaki hii na itapunguza gharama za mawasiliano kwa wateja wao wanaowasiliana kutoka nchi moja kwenda nchi nyingine kwa kuwa hadi sasa Airtel wapo nchi 16 za Afrika na wana makubaliano ya moja kwa moja ya kutumia miundombinu na huduma za mawasiliano.

Baada ya kupokea maoni ya wadau, Kakoso amesema kuwa Kamati yake imeridhia Itifaki hiyo na itawasilisha taarifa yake Bungeni na kuunga mkono Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ili Itifaki hiyo iweze kuridhiwa kupitishwa na Bunge


from MPEKUZI

Comments