Ali Kiba: Sina Ugomvi Wowote na Diamond Platnumz, Lakini Sipo Tayari Kushiriki Tamasha Lolote Atakaloliandaa

Msanii wa Bongo Fleva, Ali Kiba amesema hana ugomvi na msanii mwenzie Naseeb Abdul maarufu Diamond Platnumz kama watu wanavyoongea na anafurahia mafanikio yake anayopata kupitia muziki

Kiba amewataka Watanzania wamsapoti Diamond Platnumz kwani ni msanii mzuri na anaiwakilisha nchi vizuri

Kiba amesema hayo  katika mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika  Novemba 8, jijini Dar es Salaam ambapo amesema hana ugomvi na Diamond isipokuwa alishamwambia hatoshiriki onesho lolote atakaloandaa

“Diamond nilishamwambia sitoweza kushiriki katika onesho lolote atakalofanya, nafurahia mafanikio anayopata, kama amepata siwezi kufanya kwasababu mimi pia nina yangu ya kuyafanikisha, hakuna ugomvi kati yetu

“Nilipomjibu nikitumia mfano wa penseli nilimaanisha kuwa aache mambo ya kitoto kwasababu nilishamjibu, mimi sio mtoto mdogo sirudii tena kujibu, mimi mwanaume na mwanaume anaongea mara moja tu

“Nafurahia sana muziki wa Diamond naomba muendelee kumsapoti kwasababu ni msanii mzuri, anafanya kazi nzuri na anawakilisha nchi yetu,” amesema Kiba.

Katika hatua nyingine, Alikiba amesema atafanya  ziara aliyoiita ‘Unforgatable’ nchini nzima akiweka kambi za kupima afya kila mkoa kwa magonjwa yasiyo ya kuambukiza.
"Kwa jinsi ambavyo mashabiki wangu wamenionesha upendo kwa miaka 17, nimeamua kuwaletea Alikiba Unforgettable Tour ambayo itakuwa na mambo mengi sana haiishii tu kuwa Concert au Tour.

"Alikiba Unforgettable Tour itakuwa na mambo makubwa matatu. 1. Ujenzi wa Ndoto kazi kwa vijana, ambapo mimi na wenzangu watakaonishika mkono tutapita mikoani kuzungumza na wanafunzi wa vyuo. Jambo namba 2 kwenye Alikiba Unforgettable Tour ni Medical Camp, hapa namshukuru Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu na jopo la madaktari, ambao watatoa mchango wa dawa kwa lengo la kutoa huduma ya afya kwa watu mbalimbali bure kabisa.", ameongeza.


from MPEKUZI

Comments