Waziri Biteko Atatua Mgogoro Wa Wachimbaji Misungwi

Na Tito Mselem Mwanza,
Waziri wa Madini Doto Biteko ametatua mgogoro ulio dumu kwa muda mrefu na kuruhusu wachimbaji waendelee na shughuli za uchimbaji katika Machimbo ya wachimbaji wadogo ya Shilalo Wilayani Misungwi Mkoa wa Mwanza.

Mgogoro huo ulisababisha shughuli za uchimbaji wa madini ya dhahabu kusitishwa kutokana na sababu za kimaslahi katika madura 38 kati ya 57 yaliyoko kwenye Machimbo hayo.

Shughuli za uchimbaji wa madini ya dhahabu zilisitishwa Oktoba 7 mwaka huu na Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella, kwa muda usiojulikana kutokana na mgogoro wa umiliki wa eneo yalipo mashimo hayo ili kuweka utaratibu wa usimamizi wa mapato.

Akizungumza na wachimbaji wadogo katika mkutano wa hadhara Waziri Biteko aliwataka waache fitina, majungu na makundi huku akiwataka kufanya kazi na kushirikiana kwa pamoja kwani lengo la Serikali ni kuwafanya wanufaike na uchumi wa madini.

“Rais Dkt. John Pombe Magufuli alituteuwa tufanye kazi kubwa mbili katika sekta ya madini, tuwapatie wachimbaji wadogo maeneo ya kuchimba ili mshiriki kuinua uchumi wa nchi na tuhakikishe mnalipa kodi za Serikali ili fedha hizo zisaidie kuboresha maeneo mbalimbali kwa maslahi ya wananchi wote ikiwemo afya na elimu”.

“Lazima mfanye shughuli zenu kwa usalama lakini mtakapokuwa na migogoro hicho ni kiashiria cha uvunjifu wa amani, Serikali hatuwezi kuruhusu watu wake wakaumizana ndiyo maana Mkuu wa Mkoa alichukua jukumu la kusitisha shughuli za uchimbaji kwa muda, tumeshirikiana tumetatua mgogoro huo hivyo ninawasisitiza wachimbaji wote muachane na siasa zisizo na maana badala yake mfanye kazi na mlipe kodi ya serikali,” alisema Biteko.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella, aliwataka wachimbaji na wamiliki wa eneo hilo kuweka utaratibu wa usimamizi wa mapato ili kila mtu apate haki yake anayostahili na anufaike kutokana na mapato yanayopatikana katika machimbo hayo.

Aidha, Mmiliki wa eneo hilo Wilbert Kukwanja, alimshukuru Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mongella kwa kuwakutanisha na Waziri Biteko na kumaliza mgogoro huo kwa sababu kusitishwa kwa shughuli za uchimbaji katika machimbo hayo kuliwaathiri kiuchumi ambapo aliahidi kulinda amani katika eneo hilo na kutoruhusu migogoro kutokea tena.

Naye, Mbunge wa Jimbo la Misungwi, Charles Kitwanga aliwataka wachimbaji katika eneo hilo kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia usalama wao kwanza pamoja na kuepuka migogoro ambayo itawaletea hasara wao na familia zao endapo serikali itasitisha shughuli za uchimbaji huku akiwasisitiza kulipa kodi za serikali kila wanapozalisha.

Baadhi ya wachimbaji katika eneo hilo akiwemo Ally Bushiri na Maige Gaude, walimshukuru Rais Magufuli kwa  kuteuwa viongozi wachapa kazi kama Biteko ambae ametatua mgogoro huo kwani walikuwa wamekwishakata tamaa walidhani tatizo hilo litadumu kwa muda mrefu bila kupatiwa ufumbuzi.


from MPEKUZI

Comments