Mfanyabiashara Salum Shamte Atiwa Mbaroni Kwa Ubadhirifu wa Bilioni 54

Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Martin Shigela ameliamuru Jeshi la Polisi mkoani humo, kumshikilia Mwenyekiti wa Taasisi ya Sekta Binafsi (TPSF), Bw. Salum Shamte, kufuatia madai ya Kampuni yake ya Katani LTD kufanya ubadhirifu wa fedha za wakulima wa Mkonge, NSSF pamoja na serikali.

Wengine waliokamatwa ni Juma Shamte ambaye ni mkurugenzi mtendaji wa sasa wa Katani Limited, Fadhili Malima (mkurugenzi wa fedha), Theodora Mtejeta (ofisa uhusiano) na mjumbe wa bodi, Fatma Diwani.

Kukamatwa vigogo hao ni agizo la Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Martine Shigella kwa Kamanda wa Polisi mkoani Tanga, Edward Bukombe na Kamanda wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) mkoa, Christopher Mariba.

Shigela alitoa agizo hilo baada ya kupokea ripoti ya mkaguzi wa ndani wa serikali aliyoitoa katika mkutano wa wadau wa mkonge uliofanyika jijini Tanga, ambapo ripoti hiyo ilionyesha kuwa Kampuni hiyo ina upotevu wa zaidi ya Sh. bilioni 54.

Awali akiwasilisha ripoti ya ukaguzi huo, Mkaguzi wa Ndani Mwaandamizi Wizara ya fedha na Mipango, Idrisa Ally, alieleza kuwa ukaguzi huo ulianza Januari 22, hadi Februaru 22 mwaka huu ambpo ulihusisha  mwaka 2008 hadi 2018.

Ally alieleza kuwa kazi ya ukaguzi huo ulilenga kuangalia miamala ya Shirika la wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), wakulima na fedha za Sacos ya wakulima hao sambamba na kuangalia mikataba  iliyoingiwa na pande zote tatu.

Alieleza kuwa katika ukaguzi huo, zaidi ya Sh. bilioni 54 hazikufahamika zilipo ama matumizi yake yakiwamo madeni ya wakulima, makato ya wanachama wa NSSF, mkopo na kutolipwa kwa kodi ya serikali kwa mujibu wa taratibu.

Mkaguzi huyo alieleza yaliyojitokeza katika ukaguzi huo ni pamoja na madeni ya wakulima Sh. bilioni 29.8 ambazo hata hivyo alieleza hazikuonyeshwa kwenye taarifa za kampuni hiyo kiasi cha Sh. bilioni 1.7 za makato waliyokatwa wakulima huku Sacos ya wakulima ikiidai kampuni hiyo Sh. milioni  5.55.

Hata hivyo, ripoti ya mkaguzi huyo ilionyesha fedha zinazodaiwa na kampuni hiyo kwa wakulima ni zaidi ya Sh. bilioni 2.8.

Baada ya ripoti hiyo kuwasilishwa kwenye mkutsano huo na Mkuu wa Mkoa kutoa nafasi kwa pande zote kujieleza ndipo Mmiliki wa kampuni ya Katan Ltd, Salum Shamte alisimama na kukanusha ripoti iliyowasilishwa hiyo akidai haina usahihi zaidi, na kwamba hawakushirikishwa katika kuiandaa.

Shamte alieleza kuwa wao kama walezi wa wakulima tangu mwaka 1999 walikuwa wakiendesha kilimo cha mkataba wa kibiashara baina yao,bodi ya mkonge na wakulima.


from MPEKUZI

Comments