Waziri Wa Afya: Hakuna Ugonjwa wa Ebola Tanzania

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, amewatoa wasiwasi Watanzania juu ya uvumi wa uwepo wa Ebola Nchini Tanzania ambapo amesema mpaka sasa hakuna yeyote aliyethibitishwa kuwa na Ebola hapa Nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumamosi Septemba 14, 2019 Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu akiwa na naibu wake, Dk Faustine Ndugulile, mganga mkuu wa Serikali, Profesa Mohamed Kambi na jopo la wataalam  wa Shirika la Afya Duniani (WHO), amewataka wananchi kutokuwa na hofu yoyote.

Amebainisha kuwa taarifa za kuwepo kwa ugonjwa huo nchini zimetokana na watu wawili kudhaniwa kuwa na maambukizi ya Ebola katika miji ya Mwanza na Dar es Salaam.

“Hawa walikuwa wahisiwa lakini wizara imefanya vipimo vya maabara zaidi ya mara moja kama inavyoelekezwa na mwongozo wa WHO na kujiridhisha kwamba hawakuwa  na maambukizi ya virusi vya ebola hivyo hakuna ugonjwa huo Tanzania,” amesema Waziri Ummy


from MPEKUZI

Comments