Wanawake Wanne na Mwanaume Mmoja Wahukumia Jela Miezi 6 Kwa Kufanya Biashara ya Ukahaba

Na.Faustine Gimu Galafoni,Dodoma.
Wanawake 4 na Mwanaume mmoja anaedaiwa kuwa ni mteja wao wamehukumiwa kifungo cha miezi 6 na Mahakama ya Mwanzo Makole, Dodoma na adhabu ya viboko 3 wakati wa kuingia, kwa kujihusisha na biashara ya ukahaba kufuatia msako wa kuwakamata Wanawake wanaodaiwa kuwa ni makahaba Dodoma.

Akizungumza na waandishi wa habari Mkoani Dodoma  kamanda wa polisi Mkoa wa Dodoma Gilles Muroto  aliwataja waliokamatwa na kuhukumiwa kifungo hicho bila  faini na mmoja aliyehukumiwa miezi mitatu baada ya kukiri kosa, kuwa ni Erica George (24), Lucy Saibati (28), Joyce Ndekwa (30),Hawa Said (28), na Grolia Michael (29).

Kamanda Muroto alisema, Septemba 8, mwaka huu katika Mtaa wa Uhindini, Kata ya Viwandani, watu hao walikamatwa kwa kosa la kufanya ukahaba kinyume na kifungu cha sheria namba 176 (a), f na g cha kanuni ya adhabu ya sura ya 16.
 
Aidha, kamanda muroto amesema  mnamo tarehe 8/9/2019 katika kituo cha polisi kati Dodoma kundi kubwa la waendesha pikipiki (Bodaboda) zaidi ya 70 walivamia kituo  cha polisi  wilaya ya Dodoma na kufanya fujo wakitaka kumtoa mtuhumiwa aliye kuwa mahabusu Bwana Brazil Mjungu aliyekamatwa baada ya kusababisha ajali ya gari kumgonga mwendesha pikipiki ili wamuadhibu kwa kujichulia sheria mkononi.

Watu 20 wamekamatwa kuhusiana na tukio hilo na kufunguliwa mashtaka.
 
Katika hatua nyingine Kamanda muroto amesema wanaendelea na msako wa bodaboda wanao tumia pikipiki  za uhalifu, kwani jumla ya pikipiki 19 zimekamatwa zikidhaniwa kuwa niza uwizi na zinazotumika kufanya uhalifu.
 
Hata hivyo, Muroto amesema kuwa wanaendelea na misako katika maeneo mbalimbali ya mji wa Dodoma lengo likiwa ni kuwahakikisha kuwa raia wema hawabugudhiwi na wahalifu na wanafanya shughuli zao katika hali ya utulivu.
 
Ikumbukwe kuwa jeshi la polisi  liliwakamata na  kuwafikisha
mahakamani wanawake 15 wanaojiuza ambapo walihukumia kifungo cha miezi sita kila moja huku wanaume wanne waliosadikiwa kuwa ni wateja wao wakiachiwa baada ya kukosekana kwa ushahidi.
 
Hata hivyo Jeshi la Polisi Mkoa wa Dodoma limetoa onyo kwa wale wote watakao vunja sheria kwa makusudi kwani watakao kamatwa hatua kali zitachukuliwa dhidi yao .


from MPEKUZI

Comments