Hakimu Kortini kwa Tuhuma za Rushwa

Taasisi  ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Mkoa wa Kinondoni, jana Jumatano, Septemba 11, 2019, iliwafikisha mahakamani watuhumiwa watatu wa rushwa akiwemo Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo jijini Dar es Salaam, baada ya kukamilika kwa uchunguzi dhidi yao.

Takukuru imesema watuhumiwa hao ni Omary Mohammed Abdallah (40) aliyekuwa Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo Magomeni jijini Dar, ambaye ni mkazi wa Kijitonyama kwa kosa la kuomba na kupokea rushwa kiasi Tsh 703,000, Joseph Balongo (37) mfanyabiashara na mkazi wa Kibamba kwa kosa la kupokea rushwa ya Tsh 498,000 kinyume na sheria.
 

Watuhumiwa hao wanadaiwa kuomba na kupokea rushwa kinyume na kifungu cha 15 cha sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa namba 11/2007.

“Ilidaiwa kuwa mnamo Februari 12, 2017, Abdalah alimtaka mtoa taarifa ampe kiasi cha Sh. milioni moja ili aweze kumsadia kwenye kesi ya mirathi iliyokuwa mbele yake kinyume na utaratibu,” alisema.

Vile vile, alisema mlalamikaji alitoa taarifa Takukuru Wilaya ya Kinondoni, Machi mosi, 2017, uchunguzi ulifanyika na kubaini kuwa tuhuma hizo ni za kweli na shauri hilo kuanza upya.

“Uchunguzi dhidi ya tuhuma zote mbili umekamilika na watuhumiwa wamefikishwa katika Mahakama ya Kinondoni kujibu tuhuma zinazowakabili,” alibainisha.

Katika hatua nyingine, Takukuru imemfikisha mahakamani Katibu wa Kamati ya Upimaji wa viwanja katika Mtaa wa Nyakasangwe, Nerbert Malevu (33) kwa kuomba rushwa ya Sh. milioni 2.5 na kupokea Sh. 500,000.

Ilidaiwa kuwa mnamo Agosti 14, mwaka huu, mtuhumiwa huyo alimtaka mtoa taarifa ampatie fedha hizo ili aweze kumpatia sehemu ya kiwanja ambacho kilikuwa cha mtoa taarifa kabla ya upimaji na kwa madai kuwa sehemu ya kiwanja hicho kiligaiwa mtu mwingine baada ya upimaji.

“Mlalamikaji alitoa taarifa Takukuru na Agosti 16, mwaka huu uchunguzi ulifanyika, tuliandaa mtego wa rushwa na kumkamata mtuhumiwa Agosti 20, majira ya saa 10 eneo la Mwenge Lukani Pub, baada ya kupokea Sh. 500,000,” alisema Mnjagira.

Alisema, Takukuru mkoani humo imetoa wito kwa watumishi wa umma na sekta binafsi wanaodhani hawawezi kutoa huduma bila ya kuomba na kupokea rushwa, kwamba waache tabia hiyo kwa kuwa ni kosa la jinai.


from MPEKUZI

Comments