Watalaam wa chuo cha Oxford watoa mafunzo kwa madaktari bingwa

Wataalam kutoka Hospitali ya Chuo Kikuu cha Oxford nchini Uingereza wameanza kutoa mafunzo kwa madaktari bingwa wadamu, madaktari wasaratani na wauguzi ambao watatoa Huduma kwa wagonjwa watakaopandikizwa ULOTO mwishoni mwa mwaka huu.

Akizungumza kabla ya kufungua rasmi mafunzo ya wiki mbili, Mkuu wa Kitengo cha Mafunzo, Ushauri na Utafiti, Dkt. Faraja Chiwanga amesema kwamba mafunzo haya ni mwendelezo wa maandalizi ya kutoa Huduma ya upandikizaji ULOTO (bone marrow transplant) ambayo ilikuwa haipatikani hapa nchini kutokana na kutokuwapo kwa wataalam na ukosefu wa vifaa vya kutoa Huduma husika.

‘’Mafunzo haya yanajumuisha wauguzi zaidi ya 30 pamoja na madaktari bingwa 20 wa magonwa ya damu na saratani wa Hospitali ya Taifa Muhimbili,’’ amesema Dkt. Chiwanga kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa MNH.

Dkt. Chiwanga amefafanua kwamba mwezi Juni, mwaka huu hospitali ilipeleka wataalam 11 nchini India katika Hospitali ya Apollo iliyopo Chennai kwa kipindi cha mwezi mmoja ili kujifunza kwa vitendo jinsi ya kupandikiza ULOTO (bone marrow transplant).

Takwimuza MNH zinaonyesha kwamba wagonjwa takribani 130 hadi 140 wanahitaji Huduma ya upandikizaji ULOTO kwa mwakana kwamba zaidi ya theluthi mbili ya wagonjwa wenye tatizo la saratani hufariki dunia kwa kukosa Huduma hii. Uwapo wa Huduma hii utasaidia wananchi wengi kutibiwa hapa nchini, kujenga uwezo kwa wataalam wa ndani na kupunguza gharama kwa Serikali kupeleka wagonjwa nje ya nchi.


from MPEKUZI

Comments