Rais Magufuli Atoa Onyo Kwa Madereva Wote Nchini

Rais Magufuli amewataka madereva wanaoendesha vyombo vya usafiri wa abiria kuzingatia sheria na taratibu za usalama wa barabarani wakati wote wa safari zao.

Taarifa iliyotolewa jana Jumatano Julai 10, 2019 na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais Ikulu imesema Rais Magufuli ameyasema hayo Kijijii cha Kihanga, Wilaya ya Karagwe mkoani Kagera alipokutana na abiria na dereva wa basi dogo linalofanya safari zake kati ya kati ya Bukoba na Karagwe.

Rais Magufuli amesema ajali nyingi za barabarani husababishwa na ukiukwaji wa sheria na taratibu za usalama barabarani na kwamba jukumu la kuhakikisha sheria na taratibu hizo zinatekelezwa upo kwa watumiaji wote wa barabara hasa madereva wanaoendesha vyombo vya usafiri.

“Poleni na safari ndugu zangu, nimefurahi kuwaona na kuwasalimu, na wewe dereva hongera kwa kazi, fanya kazi zako kwa kuzingatia sheria na taratibu za usalama barabarani, pia kumbuka kusali kabla na baada ya safari” alisema Rais Magufuli

Pia, Rais Magufuli ametumia fursa hiyo kuwaeleza abiria ambao ni wanafunzi kusoma kwa juhudi masomo yao.


from MPEKUZI

Comments