Meneja wa Maabara wa Tume ya Madini Adakwa kwa tuhuma za wizi wa Madini ya serikali

Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es salaam linamshikilia Dornald Joseph Njonjo (30) Meneja wa Maabara wa Tume ya Madini kwa tuhuma za kuiba madini ya dhahabu mali ya serikali kilogram 6.244 yenye thamani ya Tsh 507,347,000/= yaliyokuwa yamehifadhiwa kwenye Kasiki katika ofisi za wakala wa madini Masaki Jijini Dar es salaam.

Mnamo tarehe 29, Juni, 2019 Jeshi la Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam lilipata taarifa kutoka kwa Ndugu ALLY SADICK(40) afisa madini Mkoa wa Dar es Salaam baada ya kugundua kuibiwa madini hayo ya dhahabu.

Jeshi la Polisi baada ya kupata taarifa hizo lilianza uchunguzi mara moja na kubaini kuwa madini hayo yaliibiwa na Dornald Joseph Njonjo na kuwa alianza kuiba tangu mwaka 2018 mwezi Desemba.

Baada ya mtuhumiwa kuhojiwa alikiri kuiba madini hayo kidogokidogo ambayo yalikuwa yamehifadhiwa kwenye chumba katika jengo la ofisi za tume ya madini zilizopo Masaki.

Mtuhumiwa alieleza kuwa madini hayo aliyauza katika duka la kuuzia vito vya dhahabu na kisha kuhifadhi madini bandia yenye uzito wa kilo 6.001 nyuma ya jengo la tume ya madini ili kuyapeleka katika chumba walichoiba madini hayo halisi ili kuyabadilisha.

Madini hayo halisi ya dhahabu yalikamatwa mwaka 2017 huko maeneo ya Bandarini Zanzibar yakiwa yanasafirishwa kinyume cha sheria kisha kuitafishwa na serikali na kuhifadhiwa katika ofisi za tume ya madini.

Jeshi la Polisi Kanda maalum ya Dar es salaam linakamilisha utaratibu wa kupeleka jalada kwa mwendesha mashtaka wa serikali ili mtuhumiwa afikishwe mahakamani.

LAZARO B. MAMBOSASA – SACP
KAMANDA WA POLISI
KANDA MAALUM DAR ES SALAM.
11.07.2019


from MPEKUZI

Comments