Wakulima Wanashindwa Kukopesheka Kwa Kukosa Elimu Ya Mikopo

Na AMIRI KILAGALILA
Wakulima Nchini wanashindwa kukopesheka kutokana na ukosefu wa elimu ya mikopo kutoka taasisi za kifedha na kupelekea kuwa na kilimo kidogo kisichokuwa na tija.

Hayo yamebainishwa mkoani Njombe na maafisa kilimo wa mkoa wa Njombe WILSON JOEL pamoja na afisa kilimo wa mkoa wa Iringa GRACE MACHA  katika warsha fupi ya wanunuzi wa mazao,wasamabazaji wa pembejeo,viongozi wa vikundi vya wakulima(vyama vya msingi vya wakulima AMCOS) pamoja na watoaji wa huduma za kifedha.

“swala kubwa ni uelewa kwenye Nyanja ya fedha kati ya benki zenyewe wao wanatizamaje kwa maana mahala pengine unakuta baadhi ya maeneo hawana uelewa wa kutosha kwenye sekta ya kilimo ndio maana inapelekea kama wakulima washindwe kukopesheka hivyo ni kweli changamoto hii ipo na muhimu nafikiri kushirikiana na kupeleka elimu kwa kuwa mikopo inawezekana kukiwepo na uelewa”alisema Wilson Joel.

JULIUS MWITA ni mrajisi msaidizi wa vyama vya ushirika mkoani Njombe amesema kuwa wakulima wengi wanakosa sifa ya kukopesheka kutokana na baadhi ya masharti ya taasisi za kifedha kuwa magumu,hivyo ametoa rai kwa wakulima na wananchi kurasimisha ardhi zao ili kuipa thamani itakayoweza kuwa msaada katika maswala ya mikopo.

“sasa hivi serikali ina mpango wa kurasimisha ardhi kwa kila maeneo ili iwe na thamani kwa ajili ya kupata hata mikopo kwa hiyo nitoe rai kwa wakulima kuzingatia swala hili ili waweze kukopesheka wakati mwingine”alisema Julius Mwita

FRANCIS MATATARA ni mmoja wa washiriki katika semina hiyo kutoka vyama  vya ushirika anasema kuwa licha ya changamoto mbali mbali zilizopo kwa wakulima vijijini anatoa rai kwa viongozi na taasisi za kifedha kuendelea kutoa elimu za mikopo ili waweze kuinuka kiuchumi.

“watoa huduma za kifedha kwetu sisi ni msaada mkubwa lakini bado wakulima hawajapewa elimu ya kutosha ndio maana wengi hushindwa kuchukua mikopo japo kuwa nina amini wapo wengi tu huko vijijini wenye uwezo wa kuchukua mikopo ili kuboresha kilimo.”alisema Matatara

Kwa upande wake DEODANT BERNAD kutoka shirika la TAPBDS katika mradi wa AGRA TIJA Tanzania linalofanya kazi katika sekta ya kilimo ndani ya mikoa mitatu kanda ya kusini yaani Iringa,Njombe na Ruvuma ambao ndio waandaaji wa warsha hiyo,ameahidi kuboresha sekta ya kilimo katika mikoa hiyo hasa kwa kushirikiana na wakulima pamoja na kuchochea upatikanaji wa huduma za kifedha kutoka kwenye mabenk.


from MPEKUZI

Comments