Waziri Mkuu: Hatutamvumilia Atakayehujumu Mkakati Wa Kufufua Zao La Michikichi

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali haitomvumia mtu yeyote atakayebainika kuhujumu mkakati wake wa kulifufua zao la michikichi nchini.

Amesema wanataka kuona wakulima zao hilo wakinufaika kama wengine wa mazao makuu ya biashara, hivyo haitomfumbia macho mtu atakayezembea.

Aliyasema hayo jana jioni (Jumapili, Februari 17) mara baada ya kukagua shamba la michikichi la kikosi cha Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) Bulombora.

Alisema Serikali inataka kuona wakulima wa zao hilo wakinufaika kama ilivyokuwa kwa wakulima wa korosho, chai, kahawa, pamba na tumbaku.

Alisema Serikali imeamua kulifufua zao hilo kwa lengo la kumaliza tatizo la upatikanaji wa mafuta ya kula kwani inatumia fedha nyingi kuagiza nje ya nchi.

Waziri Mkuu alitumia fursa hiyo kuwaagiza viongozi mkoani Kigoma kwamba suala la kilimo cha michikichi liwe ajenda ya kudumu kwenye vikao vyao.

Kadhalika, Waziri Mkuu aliiagiza Wizara ya Kilimo ianzishe shamba darasa la zao la michikichi ili wananchi waweze kujifunza mbinu bora za kulima zao hilo.

Awali, Naibu Waziri wa Kilimo, Omary Mgumba alisema Serikali imetenga zaidi ya sh. bilioni 10 kwa ajili ya kuboresha kilimo cha zao la michikicho.

Waziri huyo alisema kiasi hicho cha fedha kimetengwa katika bajeti ya wizara hiyo ya mwaka 2019/2020 kwa ajili ya kuboresha kilimo cha michikichi nchini.

Alisema iwapo kilimo cha zao hilo kitaboreshwa kitasaidia Serikali kuokoa fedha nyingi za kigeni zilizokuwa zikitumika kuagiza mafuta kutoka nje ya nchi.

Pia, Waziri Mgumba alisema tayari wizara hiyo imeshaongeza watafiti zaidi ya 10 wa zao la michikichi katika kituo cha utafiti wa zao hilo cha Kihinga.

Waziri Mgumba alipongeza Jeshi la Magereza  na JKT kwa ushirikiano wanaoutoa kwa wizara katika kipindi hiki cha ufufuaji wa zao la michikichi.

Naye Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dkt. Hussein Mwinyi alimuhakikishia Waziri Mkuu kuwa maelekezo yote aliyoyatoa kuhusu kilimo cha michikichi watayatekeleza.

(mwisho)
IMETOLEWA NA
OFISI YA WAZIRI MKUU,


from MPEKUZI

Comments