Muungano wa majimbo 16 nchini Marekani Yamshitaki Rais Donald Trump

Muungano wa majimbo 16 nchini Marekani yakiongozwa na California yameushtaki utawala wa Rais Donald Trump kuhusu uamuzi wa kutangaza hali ya dharura ili kukusanya fedha za ujenzi wa ukuta wa mpakani na Mexico.

Kesi hiyo imewasilishwa katika mahakama ya wilaya ya kaskazini katika jimbo la California. Inajiri siku kadhaa baada ya Trump kuidhinisha hali ya dharura, inayompa nguvu kulivuka bunge na kujipatia fedha kwa ujenzi huo – ambayo ni ahadi kubwa aliyotoa wakati wa kampeni yake.

Democrats wameapa kupinga hatua hiyo “kwa kutumia njia zozote zilizopo”. Mkuu wa sheria katika jimbo hilo la California, Xavier Becerra, amesema wanampeleka Trump mahakamani “kuzuia matumizi mabaya ya nguvu za rais”.

“Tunamshtaki Trump kumzuia dhidi ya kuiba pesa za mlipa kodi, zilizotengwa kisheria na bunge kwa watu wa majimbo yetu. Kwa wengi wetu, ofisi ya rais si eneo la vioja ,” aliongeza

Kesi hiyo iliyowasilishwa Jumatatu inaanza kwa kusikizwa awali ombi la kutaka kumzuia Trump ashughulikie dharura hiyo aliyoitangaza, wakati kesi ikiendelea kortini,” gazeti la Washington Post linaripoti.

Trump alitangaza mpango huo baada ya bunge kukataa kufadhili ujenzi wa ukuta. Kesi ya kwanza iliwasilishwa mara moja siku ya Ijumaa. Kundi la kutetea haki, Public Citizen, liliwasilisha kesi kwa niaba ya hifadhi asili, na wamiliki watatu wa ardhi katika jimbo la Texas ambao wamearifiwa huenda ukuta huo ukajengwa kwenye ardhi yao.

Akitoa tangazo hilo katika ikulu ya White House siku ya Ijumaa, rais amesema hali hiyo itaruhusu kupata takriban dola bilioni 8 kwa ujenzi wa ukuta huo wa mpakani. Hiki ni kiwango kilicho chini ya gharama ya jumla ya dola bilioni 23 zinazohitajika kujenga ukuta huo wenye urefu wa maili 2,000 wa mpaka huo.


from MPEKUZI

Comments