Na Amiri kilagalila
MADIWANI wa halamshauri ya Manispaa ya Iringa mkoani Iringa wameipongeza halmashauri hiyo kwa kuendelea kuongoza kitaifa katika ukusanyaji wa mapato kwa kundi la Halmashauri za Manispaa nchini .
Madiwani hao walitoa pongezi hizo jana mara baada ya taarifa ya mstahiki meya wa Manispaa ya Iringa Alex Kimbe kutoa taarifa rasmi katika kikao hicho kuhusu Manispaa ya Iringa kuongoza kwa ukusanyaji wa mapato kwa mwezi Januari .
Diwani wa kata ya Mwangata Edward Chengula alisema kuwa ni hatua ya kujipongeza kwa halmashauri hiyo ya Manispaa ya Iringa kuendelea kufanya vizuri katika ukusanyaji wa mapato na kuwa kinachoendelea ni uwajibikaji mzuri wa watendaji wa halmashauri hiyo chini ya mkurugenzi wake Hamid Njovu pamoja na madiwani .
Alisema pamoja na kufanya vizuri katika ukusanyaji wa mapato , Manispaa ya Iringa ni moja kati ya Halmashauri ambazo zimefanya vizuri katika zoezi la ujenzi wa vyumba vya madarasa na kufanikiwa kupeleka wanafunzi wote waliofaulu mtihani wa darasa la saba kujiunga na sekondari .
" Ushirikiano uliopo ndio ambao umepelekea Halmashauri yetu kuendelea kuwa wamoja na kuwatumikia wananchi kwa nguvu ya umoja bila kuwepo mivutano ya kisiasa hadi sasa mfano kata yangu ya Mwangata najivunia kuona watoto waliofaulu kujiunga na elimu ya sekondari wote wanakwenda shule ila pia kuna maendeleo makubwa yanayofanywa katika kata ya Mwangata " alisema Chengula
Naibu meya wa Manispaa ya Iringa Joseph Lyata alisema kuwa kuongoza kwa Manispaa hiyo katika ukusanyaji kodi ni ishara nzuri kuwa wananchi wa Manispaa ya Iringa wameitikia wito wa serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Rais Dkt John Magufuli ya kila mmoja kulipa kodi kwa maendeleo ya Taifa .
Naye Mbunge wa viti maalum mkoa wa Iringa, Ritta Kabati (CCM) na mbunge wa viti maalum mkoa wa Iringa, Suzana Mgonakulima (Chadema) wamesema kuwa mbali na kuipongeza manispaa yao kwa kufanya vizuri katika ukusanyaji wa mapato ila wanapongeza kwa ujenzi wa vyumba vya madarasa ambavyo vimepelekea watoto wote kwenda shule . .
from MPEKUZI
Comments
Post a Comment