Rais Magufuli amtaka Waziri Mpya wa Madini Dotto Biteko kuanzisha vituo vya madini mikoa inayofanya shughuli za uchimbaji

Rais John Magufuli amemwagiza Waziri wa Madini, Dotto Biteko kuanzisha vituo vya madini kwenye maeneo yanayozalisha migodi nchini.

Alitoa maagizo hayo baada ya kuwaapisha viongozi wapya wa serikali jana  Jumatano, Ikulu jijini Dar es Salaam. 

Rais Magufuli alieleza kuwa maagizo hayo yanalenga kudhibiti madini yanayoibwa na kupelekwa nje huku nchi kushindwa kunufaika ipasavyo.

“Ripoti mbalimbali katika nchi za Afrika Mashariki zinaonyesha Tanzania kuwa nyuma katika uuzaji wa dhahabu wakati sisi ndio tunaongoza katika uchimbaji, kwa ripoti hii ni lazima tujiulize tunakwama wapi? Dhahabu tunazochimba zinauzwa wapi? Soko lipo wapi na tunalijua? Tunapouza tunapata fedha kiasi gani? Wizara ipo na wataalamu wake na hapo ndio changamoto inapoonekana” Alisema Rais Magufuli.

Rais Magufuli aliagiza pia Waziri Biteko kushirikiana na Benki Kuu (BOT) kuweka mkakati utakaowezesha nchi kuanza kununua dhahabu na kuitunza. 

“Tanzania lazima isimame, hatuwezi kuendelea kuibiwa dhahabu, lazima tutunze dhahabu yetu, itatufaa hata shilingi yetu ikishuka,” aliongeza.


from MPEKUZI

Comments