Makamu Wa Rais Azindua Jengo Ghorofa Mbili La Kituo Cha Mama Na Mtoto

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan amewataka wanaotoa huduma katika sekta ya afya kutoa Huduma bora.

Makamu wa Rais ameyasema hayo jana wakati wa uzinduzi wa jengo la kituo cha Mama na Mtoto katika hospitali ya KMKM Kibweni ikiwa sehemu ya maadhimisho ya shamrashamra za kutimiza miaka 55 ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Makamu wa Rais ametoa rai kwa Wataalamu wa Afya nchini kutambua kuwa wanatakiwa kutumia utaalamu wao katika kuokoa maisha ya mama na mtoto ili kuepuka vifo vitokanavyo na uzazi kwa ajili ya kujenga Taifa lenye kizazi imara.

“Ni wajibu wenu kutumia utaalamu wenu na jukumu mlilopewa na Taifa katika kuleta mabadiliko ya kiutendaji na ufanisi katika sekta ya afya nchini” alisema Makamu wa Rais.

Jengo la Kituo cha Mama na Mtoto ni la ghorofa mbili na limegharimu jumla ya shilingi 3, 648,400,000/- na kuzingatia watu wenye mahitaji maalumu.

Huduma zitakazopatikana kwenye jengo hilo la ghorofa mbili ni Huduma ya Mama na Mtoto, Wodi ya Wazazi na Watoto,Huduma ya Upasuaji kwa Mama Wajawazito, Huduma ya Vipimo X Ray, Utra Sound na Maabara, Ofisi za huduma za madaktari, wauguzi na wahudumu wengineo.

Mradi huu wa ujenzi wa jengo la Mama na Mtoto ni utekelezaji kwa vitendo wa malengo halisi ya mwasisi wa Mapinduzi Matukufu za Zanzibar ya mwaka 1964 marehemu Mzee Abeid Amani Karume ambaye alidhamiria kuimarisha huduma ya Afya kwa wakulima.

Uzinduzi wa Jengo hilo umerahisisha upatikanaji wa huduma hiyo kwa wakazi wa maeneo ya Kibweni, Mwanyanya, Bububu, Mbuzini, Mtoni, Kama, Mfenesini, Mahonda, Mtopepo na maeneo mengine.

Kwa upande mwingine Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ Mhe. Haji Omar Kheir amesema Serikali itaendelea kusimamia yale yanayopaswa kutekelezwa haswa kwenye huduma za Afya.


from MPEKUZI

Comments