Diwani Ashambuliwa Kwa Mapanga

Diwani wa Sabasabini katika Halmashauri ya Ushetu, Kahama mkoani Shinyanga, Emmanuel Makashi amenusurika kifo baada ya kushambuliwa kwa kukatwa mapanga na watu wanaodaiwa kuwa ni majambazi nyumbani kwake usiku wa kuamkia jana.

Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Richard Obwao alisema katika tukio hilo, wavamizi hao walimpora diwani huyo fedha taslimu Sh5 milioni.

“Ni vyema wananchi wakajenga tabia ya kuhifadhi fedha benki badala ya kukaa majumbani na kiasi kikubwa cha fedha na hivyo kuvutia wahalifu,” alisema.

“Katika purukushani za kupora fedha hizo, diwani Makashi alijeruhiwa kwa kukatwa mapanga alipojaribu kukabiliana na wavamizi hao ambao majina wala idadi yao haijajulikana,” alisema.

Alisema wakati wakitimka mbio baada ya kupora na kujeruhi, mmoja wa watuhumiwa aliyetambuliwa kwa jina la Yohana Masanja (19), mkazi wa Kijiji cha Lowa alikamatwa na kushambuliwa hadi kufa na wananchi waliojitokeza baada ya kusikia kelele za kuomba msaada. Baada ya kumuua, wananchi hao walimteketeza kwa moto.


from MPEKUZI

Comments