CHADEMA Wapinga na Kulaani Madai ya DC Sabaya Kumnyang'anya Freeman Mbowe Ofisi ya Ubunge

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Wilaya ya Hai kimesema mkuu wa wilaya hiyo, Lengai ole Sabaya amepotosha umma kueleza kuwa amemnyang’anya ofisi mbunge wa jimbo hilo, Freeman Mbowe ilhali hajawahi kuwa na ofisi katika jengo la halmashauri hiyo.

Januari 14, Sabaya alitangaza kumnyang’anya ofisi ya ubunge Mbowe baada ya kueleza hajaitumia tangu mwaka 2010 hivyo itatumiwa na idara ya uhamiaji.

Wakizungumza katika ofisi ya mbunge huyo jana, mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Helga Mchomvu ambaye pia diwani wa Muungano alisema wanalaani kauli ya Sabaya kwa kuwa amepotosha umma.

Mchomvu alisema ofisi ya mbunge huyo ipo mji mdogo wa Bomang’ombe.

“Wananchi ondoeni hofu huduma katika ofisi ya mbunge zinaendelea kama kawaida, katibu wake yupo na ofisi haijawahi kufungwa, muda wowote wananchi njooni,” alisema.

Hata hivyo, Sabaya alipoulizwa kwa simu jana kuhusu madai hayo ya Chadema, alisema ameshafunga suala hilo hivyo wamwache aendelee na kazi za wananchi.

Mbowe yupo gerezani baada ya kufutiwa dhamana na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kwa madai kuwa alikiuka masharti ya dhamana yeye na mbunge wa Tarime Mjini, Ester Matiko.


from MPEKUZI

Comments