CHADEMA Wamvaa Spika Ndugai Sakata la Ubunge wa Tundu Lissu

Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimeamua kuingilia kati kufuatia kauli ya Spika wa Bunge wa Job Ndugai kumtaka Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu lissu arudi nchini kwa kuwa hana ruhusa ya kuwa huko

Akizungumzia kauli hiyo ya Spika Ndugai, Mkurugenzi wa Mawasiliano, Itikadi na Mambo ya Nje wa CHADEMA John Mrema amesema kauli ya Spika haina tija kwa kuwa Tundu Lissu bado hajapewa ruhusa na Daktari wake kurejea nchini kwa madai kuwa amepona kabisa.

"Spika si Daktari mpaka aseme kuwa Lissu amepona na hajawahi kumtembelea kwa kipindi chote tokea apelekwe hospitali. 

"Tunakumbuka aliyewahi kuwa waziri wakati wa serikali ya awamu ya nne, Prof. Mwandosya aliugua kwa zaidi ya mwaka, lakini hatukusikia kauli za aina hii." Amesema Mrema.

Alipoulizwa  kwa nini Tundu Lissu ameanza kutembelea nchi kama Uingereza, aliyoitembelea wiki iliyopita, ilhali bado ni mgonjwa, Mrema alisema Ubelgiji na Uingereza si mbali kwa kuwa ni saa moja tu kwa usafiri wa ndege.

Jana Spika Ndugai alimtaka Mbunge Tundu Lissu huyo kurejea nchini ili kuendelea na shughuli za Bunge kwa kuwa hana kibali cha kuwa nje ya nchi.

Spika Ndugai aliongeza Lissu hana ruhusa ya kuwa nje ya Bunge, hivyo anatakiwa kurejea nchini kuendelea na shughuli za ubunge.


from MPEKUZI

Comments