Mabadiliko ya Rangi Katika Bendera ya Taifa na Wimbo wa Taifa

Wizara  ya Mambo ya Ndani ya Nchi, imetoa maelekezo juu ya matumizi ya wimbo wa taifa na mabadiliko ya rangi ya bendera ya taifa kuwa itakuwa ya dhahabu na si manjano kama ilivyozoeleka.

Hayo yamebainika baada ya wizara kutoa maagizo kwa vyuo na taasisi kuhusiana na matumizi ya tunu hizo za taifa.

Pia barua hiyo ilisisitiza kuwa rangi sahihi za bendera ya taifa kuwa ni kijani, dhahabu, nyeusi na bluu na kusisitiza kwamba ni makosa kutumia rangi ya njano.

Maelekezo hayo yametolewa kwa wakuu wa vyuo vya ualimu, vyuo vya maendeleo ya jamii, wakuu wa vyuo vikuu na vyuo vikuu vishiriki na taasisi zilizo chini ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Kwa mujibu wa barua hiyo, iliyotolewa Novemba 23, mwaka huu na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, ambayo jana ilisambaa kwenye mitandao ya kijamii, maelekezo hayo yameletwa kwa sababu imebainika kuwa taasisi za serikali zinatumia isivyo sahihi alama za taifa.

Ofisa Habari wa Wizara ya Elimu, Mwasu Sware, alithibitisha kwamba barua hiyo ni yao na kuomba watafute Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kwa maelezo zaidi ya kwa nini imesambaa mtandaoni.
 
Barua hiyo ambayo iliandikwa na wizara ikiwa na muhuri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, ilisema Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, inaelekeza kuwa Wimbo wa Taifa utapigwa kwa dhifa za kitaifa pekee.

“Endapo hadhi ya sherehe haitambuliki, taasisi inalazimika kuomba kibali kwa waziri mwenye dhamana. Wimbo unatakiwa kuimbwa kwa ukamilifu beti zote mbili kwa kuzingatia ‘nota’ na maneno.

Kadhalika barua hiyo ilisema kuwa uwiano wa bendera ni theluthi katika urefu na upana.



from MPEKUZI

Comments