Kesi ya Zitto Kabwe Kuchukua Mashahidi 15

Mashahidi 15 kutokea Upande wa Mashtaka wanatarajiwa kutoa ushahidi wao katika kesi ya uchochezi inayomkabili mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe.

Hayo yameelezwa na Wakili Serikali, Wankyo Simon mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi baada ya kumaliza kumsomea Zitto maelezo ya awali (Ph).

Akisoma Maelezo ya awali ya kesi hiyo, Wankyo amedai Oktoba 28, 2018 mshtakiwa akiwa katika mkutano na waandishi wa habari, uliofanyika katika Makao Mkuu ya Ofisi ya Chama cha ACT-Wazalendo, Kijitonyama jijini Dar es Salaam alitoa maneno ya uchochezi yenye kuleta hisia ya hofu na chuki.

Amesema kuwa Zitto alianza kwa kudai kuwa, anamnukuu…. “Watu ambao walikuwa ni majeruni katika tukio la mapambano baina ya wananchi na polisi wakiwa wamekwenda kupata matibabu katika kituo cha Afya Nguruka, polisi wakapata taarifa kuwa kuna watu wanne wamekwenda kituo cha afya Nguruka kupata matibabu wakawafuata kule wakawaua.” Mwisho wa Kunukuu.

Wankyo amedai kuwa maneno hayo sio tu yalichochea chuki lakini pia yalitengeneza uhasama kwenye mamlaka halali na kusababisha mijadala miongoni mwa makundi mbali mbali katika jamii na kwenye mitandao ya kijamii na vyombo vya habari kwa ujumla.

Wankyo amesema Zitto alikamatwa Oktoba 30, mwaka huu akiwa nyumbani kwake Masaki, Dar na kuwekwa mahabausu ya polisi na pia nakala ya taarifa ya vyombo vya habari polisi wali ikuchukua baada ya kuwa Zitto amekamatwa. Baada ya Saimon kumaliza kumsomea maelezo hayo, Zitto alikubali majina yake, alikubali kuwa yeye ni Mbunge na pia alikubali kuwa alikamatwa nyumbani kwake Masaki.

Hata hivyo alikataa kuwa yeye si Mwenyekiti wa ACT Wazalendo na nakala ya taarifa hiyo haikukutwa nyumbani kwake wakati anakamatwa. Pia, Zitto aliyakana maelezo mengine yote aliyosomewa mahakamani hapo.  Kesi imeahirishwa hadi Januari14, 2019 kwa ajili ya kutajwa na itaendelea kusikilizwa Januari 29, 2019.


from MPEKUZI

Comments